Iran na Syria zasisitizia suala la umoja wa Waislamu
Mkuu wa Baraza la Stratijia za Uhusiano wa Kigeni wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran na Mufti Mkuu wa Syria wamesisitizia suala la umoja miongoni mwa Waislamu.
Dakta Kammal Kharrazi na Sheikh Ahmad Badreddin Hassoun wamesisitiza hilo katika mazungumzo yao katika mji mkuu wa Syria Damascus.
Dakta Kammal Kharrazi ambaye pia ni waziri wa zamani wa Mashauri ya Kigeni wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ameitaja nafasi muhimu na yenye taathira ya Mufti wa Syria katika kuleta umoja na mshikamano miongoni mwa Waislamu wa Mashariki ya Kati na kusema kwamba, mtazamo wa kukurubisha pamoja madhehebu za Kiislamu una umuhimu na taathira kubwa.

Mkuu wa Baraza la Stratijia za Uhusiano wa Kigeni wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesema kwamba, ana matumaini mtazamo wa kudumisha umoja uliopo baina ya wananchi na maulamaa wa Syria utaendelea.
Kwa upande wake Sheikh Ahmad Badreddin Hassoun, Mufti Mkuu wa Syria ameisifu Jamhuri ya Kiislamu ya Iran kwa msaada wake wa kupatiwa ufumbuzi mgogoro wa Syria na kueleza kwamba, nchi hiyo ya Kiarabu imeweza kuvuka vizuri kipindi cha vita na mgogoro na kwa sasa Damascus inataka amani na utulivu vitawale katika eneo la Mashariki ya Kati.
Aidha amesema kuwa, kumekuwa kukifanyika vikao vizuri vya kielimu mjini Tehran vyenye lengo la kukurubisha madhehebu za Kiislamu na kwamba, ana matumaini vikao hivyo vitakuwa na taathira chanya pia kwa Waislamu wote ulimwenguni.