Human Rights Watch yakosoa kamatakamata ya wanaharakati nchini Saudia
https://parstoday.ir/sw/news/west_asia-i59816-human_rights_watch_yakosoa_kamatakamata_ya_wanaharakati_nchini_saudia
Shirika la kutetea haki za binadamu la Human Rights Watch limetoa taarifa likikosoa hatua ya serikali ya Saudi Arabia ya kuwatia nguvuni maafisa wa serikali, wanaharakati na wakosoaji wa utawala wa nchi hiyo.
(last modified 2023-11-27T08:44:11+00:00 )
Mar 18, 2020 03:57 UTC
  • Saudi Arabia
    Saudi Arabia

Shirika la kutetea haki za binadamu la Human Rights Watch limetoa taarifa likikosoa hatua ya serikali ya Saudi Arabia ya kuwatia nguvuni maafisa wa serikali, wanaharakati na wakosoaji wa utawala wa nchi hiyo.

Taarifa iliyotolewa na Human Rights Watch imesema kuwa, kutiwa nguvuni watu wasiopungua 298 nchini Saudi Arabia katika siku chache za hivi karibuni kumezidisha wasiwasi kuhusu ukiukaji wa haki za binadamu nchini humo. 

Taarifa hiyo imeitaka serikali ya kifalme ya Saudi Arabia kutangaza haraka tuhuma zinazowakabili mahabusu hao.

Human Rights Watch imesema kuwa suala la kupambana na ufisadi halipasi kufanywa kisingizio cha kuhalalisha ukiukaji wa sheria na haki za binadamu nchini Saudi Arabia.  

Jumapili iliyopita vyombo vya habari vya Saudi Arabia viliripoti kuwa, maafisa 298 wa nchi hiyo wakiwemo maafisa kadhaa wa jeshi na polisi wametiwa nguvuni kwa tuhuma za ufisadi na kutumia vibaya madaraka na vyeo vyao. 

Baadhi ya wapinzani wa utawala wa kifalme wa Saudi Arabia wamenyongwa au kukatwa vichwa

Mrithi wa ufalme wa Saudia mwanamfalme Muhammad bin Salman pia amemuru kukamatwa mamia ya maafisa wa serikali, wanaharakati wa masuala ya kisiasa, mashekhe na viongozi wa dini na hata wanamfalme kadhaa wa nchi hiyo kwa tuhuma mbalimbali zikiwemo za ufisadi na kupinga utawala wa kifalme wa nchi hiyo.