Umoja wa Mataifa: Hali ya kibinadamu Yemen ni mbaya mno
Msemaji wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa amesisitiza kuwa, Yemen ingali inakabiliwa na hali mbaya mno ya kibinadamu ulimwenguni.
Farhan Haq ameashiria wahanga wa mashambulio ya hivi karibuni ya muungano vamizi unaoongozwa na Saudi Arabia na kusema kuwa, wafanyakazi wa umoja huo wamesema kuwa, watoto 9 wadogo waliuawa katika mashambulio hayo ya anga dhidi ya mji wa al-Jawf na kwamba, watoto wengine saba na wanawake wawili walijeruhiwa.
Lise Grande, mratibu wa masuala ya kibinadamu wa Umoja wa Mataifa nchini Yemen naye ameashiria mauaji hayo ya Saudia na kutoa mkono wa pole kwa familia zilizopoteza watoto wao waliouawa katika mashambulio hayo ya anga ya hivi karibuni ya Saudia.
Hivi karibuni ndege za kivita za Saudia zilidondosha mabomu katika makazi ya raia huko al-Jawf kaskazini mwa Yemen na kuwauwa watoto wadogo 9 na kujeruhi wengine kadhaa..
Duru mbalimbali za kienewo na kimataifa zimeendelea kulaani mauaji hayo ya majeshi vamizi ya muungano unaoongozwa na Saudia dhidi ya watoto wadogo wa Yemen wasio na hatia yoyote na kuutaka Umoja wa Mataifa uchukue hatua za maana dhidi ya Saudia badala ya kulaani tu kwa maneno matupu jinai za aal Saud huko Yemen.
Saudia ilianzisha mashambulizi dhidi ya Yemen mwishoni mwa mwezi Machi 2015 kwa lengo la kuiondoa madarakani Harakati ya Ansarullah na kumrejesha madarakani Abdrabbuh Mansour Hadi, rais wa zamani wa nchi hiyo aliyejiuzulu na kukimbilia Riyadh. hata hivyo hadi sasa Saudia na washiirika wakke wameshindwa kufikia malengo yao kutokana na kusimama kidete wananchi wa Yemen.