Rais wa Mexico akosoa misaada ya kijeshi ya US kwa Ukraine
https://parstoday.ir/sw/news/world-i103026-rais_wa_mexico_akosoa_misaada_ya_kijeshi_ya_us_kwa_ukraine
Rais Andrés Manuel López Obrador wa Mexico ameikosoa vikali Marekani kwa kutumia mabilioni ya dola kuisheheneza kwa silaha Ukraine.
(last modified 2025-10-23T11:19:28+00:00 )
Oct 04, 2023 03:09 UTC
  • Rais Andrés Manuel López Obrador wa Mexico
    Rais Andrés Manuel López Obrador wa Mexico

Rais Andrés Manuel López Obrador wa Mexico ameikosoa vikali Marekani kwa kutumia mabilioni ya dola kuisheheneza kwa silaha Ukraine.

Amesema Marekani inapasa kutumia fedha hizo kusaidia kupunguza na kudhibiti mgogoro wa wakimbizi katika nchi za Amerika ya Latini.

Rais López Obrador ameeleza bayana kuwa, hatua ya Marekani kutumia hadi dola bilioni 50 kwa ajili ya vita vya Ukraine haina mantiki yoyote, na badala yake ina madhara makubwa.

Wamagharibi wakiongozwa na Marekani wameendelea kuimiminia silaha Ukraine zikiwemo zilizopigwa marufuku kimataifa. 

Umoja wa Mataifa hivi karibuni ulisema umetiwa wasiwasi na tangazo la Wizara ya Ulinzi ya Marekani, kwamba Washington itaipelekea Ukraine risasi zenye madini ya urani iliyohafifishwa.

Silaha za US nchini Ukraine

Rais wa Mexico ameeleza bayana kuwa, "(Wamarekani) wametenga pesa ngapi kwa ajili ya vita vya Ukraine? Bilioni 30 hadi 50...hiki ndicho kitu kisichokuwa na mantiki zaidi kuwahi kufanywa."

Weledi wa mambo wanasema kuwa, iwapo Russia itashinda vita vya Ukraine licha ya misaada yote iliyopewa serikali ya Kyiv na nchi za Magharibi zikiongozwa na Marekani, itakuwa ni pigo kubwa kwa jeshi la nchi za Magharibi NATO na ushawishi wa Russia kimataifa utaongezeka mno.