Msemaji wa Umoja wa Mataifa: Hakuna shule zilizobakia Ukanda wa Gaza
Msemaji wa Umoja wa Mataifa amesema kuwa ikiwa ni mwanzo wa mwaka wa masomo katika Ukanda wa Gaza, zaidi ya vijana 600,000 wamenyimwa fursa ya kupata elimu rasmi kwa mwaka mwingine, na kuwa hakuna shule zinazopatikana katika ukanda huo.
Akifafanua suala hilo Stephan Dujarric, Msemaji wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa amesema kuwa shule nyingi kati ya 200 zinazoendeshwa na shirika hilo katika Ukanda wa Gaza zimekuwa makazi ya wakimbizi wa Kipalestina.
Amesema mpango wa chanjo ya polio katika Ukanda wa Gaza unaendelea chini ya usimamizi wa Umoja wa Mataifa.
Msemaji huyo wa Umoja wa Mataifa ameongeza kuwa kusimamishwa magari ya Umoja wa Mataifa na askari wa utawala wa Kizayuni katika Ukanda wa Gaza pia kunachunguzwa zaidi.
Jeshi la utawala katili wa Israel ambalo linaendeleza mauaji ya halaiki huko Gaza, siku ya Jumatatu tarehe 9 Septemba, lilisimamisha msafara wa magari ya Umoja wa Mataifa kaskazini mwa Ukanda wa Gaza kwa madai kuwa baadhi ya "washukiwa wa Kipalestina" walikuwa kwenye msafara huo.
Antonio Guterres, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa amesema hajawahi kuona kiwango kama hicho cha mauaji na uharibifu na kuongeza kuwa Umoja wa Mataifa umependekeza kusimamia usitishaji vita wowote utakaofikiwa katika Ukanda wa Gaza.
Utawala katili wa Israel ulianzisha vita vya mauaji ya kimbari dhidi ya watu wa Ukanda wa Gaza tangu tarehe 7 Oktoba mwaka jana.
Katika kipindi hiki, asilimia 70 ya nyumba na miundombinu ya ukanda wa Gaza imeharibiwa vibaya, ambapo mzingiro na mzozo mkubwa wa kibinadamu pamoja na njaa kali ya kulazimishwa, vinatishia maisha ya wakaazi wa eneo hilo.
Wizara ya Afya ya Palestina imetangaza katika takwimu zake za hivi karibuni kwamba watu elfu 40 972 wameuawa shahidi na wengine elfu 94 761 wamejeruhiwa katika mashambulizi ya kinyama ya jeshi la utawala huo dhalimu kwenye maeneo tofauti ya Gaza.