China yaipa sharti Marekani kumuuzulu kamanda wake, mkabala na kuishinikiza Pyongyang
China imempa sharti Rais Donald Trump wa Marekani la kumuuzulu kamanda wa vikosi vya nchi hiyo vilivyoko Korea Kusini mkabala na Beijing kuishinikiza Korea Kaskazini.
Gazeti la Japan la The Japan Times limeandika kuwa, serikali ya Beijing imeiwekea sharti Washington la kumuuzulu Adimeri Harry Harris, kamanda wa vikosi vya Marekani vilivyoko nchini Korea Kusini, mkabala na kutekeleza pendekezo la Rais Tump la kuiwekea mashinikizo serikali ya Pyongyang.
Harris anatambuliwa na China kama mtu mwenye misimamo mikali sana dhidi ya Beijing na Pyongyang. Kwa mujibu wa gazeti la The Japan Times pendekezo hilo la Uchina limetupiliwa mbali na Rais Donald Trump. Adimeri Harry Harris, ndiye aliyetoa amri ya moja kwa moja ya kutumwa meli ya kijeshi ya kubeba ndege za vita ya USS Carl Vinson kwenda katika maji ya Peninsula ya Korea kama ambavyo pia ni muhusika mkuu wa kuongezeka mivutano katika eneo hilo. Kadhalika Harry Harris aliyezaliwa Japan na kukulia Marekani, ana nafasi kubwa katika kuidhaminia usalama Marekani eneo la Asia mashariki.
Gazeti la The Japan Times limefafanua kuwa, kamanda huyo mwenye misimamo ya kuchupa mipaka ndiye aliyetoa pendekezo la kuwekwa ngao ya makombora ya Marekani aina ya THAAD nchini Korea Kusini ambayo imekabiliwa na upinzani mkubwa wa China, Russia na Korea Kaskazini. Hivi karibuni serikali ya Korea Kaskazini iliionya China kwamba ikiwa itaiwekea mashinikizo yoyote, basi Pyongyang haitachelewa kukata mahusiano baina yake na Beijing.