Russia: Marekani inataka kuikalia kwa muda mrefu nchi ya Syria
Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Russia ametangaza kuwa, Marekani imeazimia kubakia Syria kwa muda mrefu kwa kutumia visingizio mbalimbali.
Maria Zakharova amesema kuwa, Marekani imeazimia hasa kuishambulia Syria na kwamba Miscow inaamini kuwa, madai yanayotolewa na Washington kwamba kuna hatari serikali ya Syria ikafanya shambulio la silaha za kemikali ni ya uwongo.
Bi Zakharova ameongeza kuwa, Washington imetangaza kuwa, kuna uwezekano wanajeshi wake wakaendelea kuwepo nchini Syria baada ya kuangamizwa kundi la Daesh kwa kisingizio cha kusaidia kutatua hitilafu baina ya vikosi vya serikali ya Syria na makundi yenye silaha yanayoungwa mkono na Washington nchini humo.
kabla ya hapo, Nick Halley Mwakilishi wa Kudumu wa Marekani katika Umoja wa Mataifa aliashiria pia uamuzi wa nchi yake wa kubaki huko Syria.
Kuwepo wanajeshi wa Marekani na kuendelezwa mashambulizi ya muungano eti wa kupambana dhidi ya Daesh huko Syria chini ya uongozi wa Marekani, hadi sasa hakujakuwa na matunda yoyote ghairi ya kuua raia madhulumu wa Syria na kuwafanya wengine kuwa wakimbizi sambamba na kuharibu miundo mbinu ya nchi hiyo.