Papa Francis awaunga mkono raia wa Venezuela
(last modified Fri, 25 Jan 2019 08:11:10 GMT )
Jan 25, 2019 08:11 UTC
  • Papa Francis awaunga mkono raia wa Venezuela

Kiongozi wa Kanisa Katoliki Duniani Papa Francis amewataka walimwengu kuwaepushia matatizo zaidi raia wa Venezuela.

Alessandro Gisotti, Msemaji wa Muda wa Vatican nchini Panama amesema kuwa, kiongozi huyo wa Kanisa Katoliki Duniani anaunga mkono juhudi zote zenye lengo la kuepusha kuwatwisha matatizo zaidi raia wa Venezuela. Papa Francis ambaye yuko nchini Panama kwa ajili ya mkutano wa maaskofu wa Amerika ya Kati amesisitizia udharura wa kuhitimishwa migogoro ukiwemo mgogoro wa kiuchumi na ukosefu wa chakula kwa ajili ya raia wa Venezuela.

Papa Francis, Kiongozi wa Kanisa Katoliki Duniani

Nchi hiyo ambayo inapinga siasa za kibeberu za Marekani huko katika eneo la Amerika ya Latini na ambayo inakabiliwa na vikwazo vya kiuchumi na vitisho vya kiusalama na kijeshi kutoka Washington, hivi sasa imetumbukia katika mzozo mkubwa baada ya Washington kutangaza kumuunga mkono kiongozi wa upinzani, Juan Guaido, spika wa bunge aliyefutwa kazi aliyejitangaza kuwa rais wa muda wa nchi hiyo. Kufuatia matukio hayo yaliyochochewa na Marekani, Uingereza na baadhi ya nchi za Ulaya, baadhi ya nchi za eneo kama vile Canada, Brazil, Paraguay, Chile na Argentina, zimetangaza kumuunga mkono kiongozi huyo wa upinzani, huku nchi zingine kama vile Jamhuri ya Kiislamu ya Iran, Mexico, Bolivia, Cuba, Uturuki, China na Russia zikitangaza kumuunga mkono Rais Nicolás Maduro wa nchi hiyo. Hii ni katika hali ambayo Maduro amewataka wananchi wa nchi hiyo wawe macho na wachukue tahadhari kubwa katika kipindi hiki kigumu ambacho nchi hiyo inapambana na njama za kila upande hasa kutoka kwa Marekani.

Tags