Jun 11, 2016 15:29 UTC
  • Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa laazimia kuangamiza Ukimwi Duniani

Mkutano wa ngazi ya juu wa siku tatu wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa kuhusu namna ya kukomesha maambukizi ya Ukimwi umefungwa mjini New York.

Mkutano huo uliomalizika Ijumaa uliwaleta pamoja, mawaziri wa afya kutoka nchi wanachama wa Umoja wa Mataifa, asasi za kiraia, wanaharakati wa kukabiliana na Ukimwi, mashirika ya Umoja wa Mataifa na wadau wengine.

Mjadala ulijikita katika umuhimu wa kuongeza juhudi za vita dhidi ya ukimwi kwa miaka mitano ijayo ili kuiweka dunia katika msitari wa kutokomeza kabisa maradhi hayo ifikapo mwaka 2030 katika sehemu ya utekelezaji wa malengo ya maendeleo endelevu SDG’s.

Kenya kwenye mkutano huo iliwakilishwa na Waziri wa Afya Daktari Cleopa Mailu ambaye alisema maambukizi ya Ukimwi nchini humo yamepungua kutoka asilimia 14 hadi sita.

Naye Naibu Waziri wa Afya wa Tanzania Daktari Hamis Kigwangalla aliyeiwakilisha nchi yake katika kikao hicho amesema, Tanzania imepiga hatua kubwa katika vita dhidi ya ukimwi, lakini mafanikio hayo hayatakuwa na maana endapo jitihada zilizopo zitadorora.

Tags