Joseph Kabila kuitembelea Goma hivi karibuni
Joseph Kabila Rais wa zamani wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo amesema anapanga hivi karibuni kutembelea mji wa Goma unaodhibitiwa na waasi wa M23 wanaoungwa mkono na Rwanda.
Kabila amesema serikali ya sasa ya Congo ni ya kidikteta baada ya bunge kumuondolea kinga na kufungua njia ya kiongozi huyo wa zamani aliye na miaka 53 kushitakiwa dhidi ya tuhuma za uhalifu wa kivita, uhaini na kushiriki katika harakati za uasi.
Katika hotuba yake iliyopeperushwa moja kwa moja kupitia mitandao ya kijamii, Kabila aliyeiongoza Kongo kuanzia mwaka 2001 hadi 2019 amemlaumu rais wa sasa Felix Tshisekedi ambaye awali alidai Kabila anashirikiana na waasi wa M23.
Kabila alisema kutokana na fununu za kwamba tayari ameutembelea mji wa Goma serikali ya Kongo imechukua ''uamuzi wa kiholela'' wa kumuondolea kinga.
"Siku chache zilizopita kufuatia uvumi kutoka mitaani au mitandaoni kuhusu madai ya kuwepo kwangu Goma, ambako nitaenda katika siku zijazo, kama ilivyotangazwa, utawala mjini Kinshasa ulichukua maamuzi ya kiholela ya kizembe bila kufikiria, na hii inaonesha kupungua kwa demokrasia nchini humo," alisema Kabila
Katika hotuba yake hiyo Joseh kabila alisema ni lazima udikteta ukomeshwe Kongo. Akisistiza kwamba demokrasia, hali nzuri ya uchumi na utawala unaowajali watu urejeshwe nchini humo.
Kabla amesema hayo saa chache baada ya Bunge la Seneti la nchi hiyo kumuondolea kinga ya kutoshtakiwa, na kufungua njia ya mwanasiasa huyo kufunguliwa mashtaka.