Waasi 148 wajisalimisha kwa serikali nchini Ethiopia
Serikali ya Ethiopia imetangaza habari ya kujisalimisha waasi 148 kwa vikosi vya usalama vya nchi hiyo.
Serikali hiyo ilitangaza jana kwamba, waasi hao ni kutoka kundi lijulikanalo kwa jina la Harakati ya Ukombozi wa Wananchi wa Gambella (GPLM).
Gat Luack, Mkuu wa jimbo la Gambella amethibitisha habari hiyo na kusema kuwa, waasi hao walikuweko katika nchi jirani ya Eritrea na sasa wameamua kurudi Ethiopia kushiriki katika ujenzi wa nchi yao.
Ertirea ilijitenga na Ethiopia baada ya kura ya maoni ya mwaka 1993. Tangu wakati huo hadi hivi sasa nchi hizo zimekuwa na ugomvi wa kila namna ukiwemo wa kugombaniana maeneo ya mpakani. Ugomvi baina ya nchi hizo mbili ni mkubwa kiasi kwamba hadi sasa umeshapelekea kutokea vita mara mbili baina yao, mwaka 1998 na 2000.
Wanamgambo wanaopinga serikali za nchi hizo mbili nao wamekuwa wakitumia maeneo ya mpakani kufanya mashambulizi ya mara kwa mara.
Ripoti zinasema kuwa, hadi hivi sasa zaidi ya watu 70 elfu wamekuwa wahanga wa mapigano baina ya nchi hizo mbili.