Makumi ya mamluki wa Sudan wauawa Yemen
Makumi ya mamluki wa Sudan waliokodishwa na Saudi Arabia wameuawa na vikosi vya kujitolea vya wananchi wa Yemen ndani ya ardhi ya nchi hiyo ya Kiarabu.
Kanali ya televisheni ya al-Masirah inayorusha matangazo yake kwa lugha ya Kiarabu imeripoti kuwa, mamluki hao wa Sudan waliuawa jana Jumamosi baada ya msafara wa magari yao kuvamiwa na vikosi vya Yemen, katika mkoa wa Hajjah kaskazini magharibi mwa Yemen.
Mbali na wanajeshi wa Sudan kupata hasara kubwa katika tukio hilo katika jangwa la Midi mkoani Hajjah, idadi kubwa ya silaha za Saudia vikiwemo vifaru zimenaswa.
Mapema jana pia, idadi kubwa ya wanajeshi wa Saudia waliuawa baada ya gari lao kulengwa na roketi aina ya Katyusha lililovurumishwa na wanamapambano wa Ansarullah kuelekea eneo la Jizan, kusini magharibi mwa ardhi ya utawala huo.
Zaidi ya Waislamu 36 elfu wa Yemen wameshauawa, makumi ya maelfu ya wengine wajeruhiwa na mamilioni ya Waislamu wengine wamekimbia makazi yao katika mashambulizi ya mungano vamizi wa kijeshi unaoongozwa na Saudia dhidi ya Yemen, kwa zaidi ya miaka mitatu sasa.