Nchi za Magharibi mwa Afrika zakata uhusiano wao na Mali
Jumuiya ya Kiuchumi ya Nchi za Magharini mwa Afrika (ECOWAS) yenye wanachama 15 imechukua uamuzi wa kufunga mipaka ya nchi hizo na Mali na kukata uhusiano wa kidiplomasia na serikali ya Bamako.
Uamuzi huo umechukuliwa baada ya serikali ya muda ya Mali kuahirisha uchaguzi mkuu uliokuwa umepanga kufanyika Februari mwaka huu hadi Disemba mwaka 2025. Msimamo huo mkali wa ECOWAS iliyotishia kuiweka Mali vikwao vikali vya kiuchumi umechukuliwa baada ya wanajeshi waliotwaa madaraka mwaka 2020 kukiuka makubaliano yake na jumuiya hiyo ya kuitisha uchaguzi mkuu mwaka huu.
Taarifa iliyotolewa na ECOWAS imesema pendekezo la kuahirishwa uchaguzi lililotolewa na serikali ya mpito ya Mali halikubaliki.
Taarifa hiyo imesema kuwa, uamuzi huo wa serikali ya mpito utakuwa na maana kwamba serikali isiyo halali ya kijeshi inawashikilia mateka watu wa Mali.
Agosti mwaka 2020 Kanali Assimi Goita aliongoza mapinduzi ya wakati yeye na maafisa wengine wa jeshi walipomuondoa madarakani Rais aliyekuwa amechaguliwa na wananchi Ibrahim Boubacar Keita baada ya maandamano ya wiki kadhaa juu ya ufisadi na mzozo wa muda mrefu wa magaidi wakufurishaji.
Awali Goita aliahidi kurejesha serikali ya kiraia Februari mwaka huu wa 2022 baada ya uchaguzi wa rais na wabunge, lakini Mei 2021 ilifanya mapinduzi ya pili na kuiondoa madarakani serikali ya muda.