Ethiopia yatangaza kusitisha vita kwa sababu za kibinadamu huko Tigray
https://parstoday.ir/sw/news/africa-i81760-ethiopia_yatangaza_kusitisha_vita_kwa_sababu_za_kibinadamu_huko_tigray
Serikali ya Ethiopia imetangaza kuhitimisha haraka vita vya ndani vya miezi 16 ili kuruhusu misaada ya kibinadamu kuingia katika eneo la Tigray lililoathiriwa na mapigaohuko kaskazini mwa nchi hiyo.
(last modified 2023-11-27T08:44:11+00:00 )
Mar 25, 2022 03:28 UTC
  • Ethiopia yatangaza kusitisha vita kwa sababu za kibinadamu huko Tigray

Serikali ya Ethiopia imetangaza kuhitimisha haraka vita vya ndani vya miezi 16 ili kuruhusu misaada ya kibinadamu kuingia katika eneo la Tigray lililoathiriwa na mapigaohuko kaskazini mwa nchi hiyo.

Idara ya Mawasiliano ya Serikali ya Ethiopia jana ilitoa taarifa ikieleza kuwa: Serikali inazitolea mwito nchi wafadhili kuzidisha misaada yao ya kibinadamu ili kupunguza hali mbaya ya watu wa Tigray. Serikali ya Ethiopia aidha imewataka wapiganaji wa Tigray waruhusu kutekelezwa mwafaka huo wa kibinadamu katika eneo hilo.   

Hata hivyo hadi sasa bado haijafahamika kama muafaka huo wa kibinadamu huko Tigray ni hatua moja kuelekea kwenye makubaliano makubwa ya kuhitimisha vita katika eneo hilo. 

Serikali ya Ethiopia imekuwa ikikabiliwa na mashinikio makubwa ya kimataifa ili kulegeza vizuizi vyake na hivyo kuruhusu misaada ya kibinadamu kuingizwa katika eneo hilo. Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Afya Duniani, Dakta Tedross Adhanom Ghebreyesus raia wa Ethiopia ambaye analihesabu eneo la Tigray kama nyumbani kwake mara kadhaa amewaomba viongozi wa Addis Ababa waruhusu kufikishwa misaada ya kibinadamu katika eneo hilo.

Tangu mwezi Novemba mwaka juzi eneo la Tigray limekumbwa na hitilafu na mivutano ya kisiasa kati ya  serikali ya Waziri Mkuu Abiy Ahmed na viongozi wa eneo hilo ambao wakati fulani waliongoza serikali ya Ethiopia. 

Abiy Ahmed, Waziri Mkuu wa Ethiopia 

Vita vilivyoshuhudiwa katika eneo hilo hadi sasa vimesababisha kuuliwa makumi ya maelfu ya watu na kupelekea mamilioni ya wengine kuwa wakimbizi.