Saudia imechukua hatua dhidi ya dini kuwazuia Mahujaji Wairani mwaka huu
Mkuu wa Chuo cha Kiislamu cha Thaqalyn mjini Kano, kaskazni mwa Nigeria amesema hatua ya utawala wa Saudia kuwazuia mahujaji Wairani mwaka huu ni kitendo kilicho dhidi ya dini na mantiki.
Katika mahojiano na shirika la utangazaji la IRIB, Shaykh Muadh Khidr amekosoa vikali uamuzi wa Saudia kuwazuia Wairani kutekeleza ibada ya Hija mwaka huu na kusema: "Ibada ya Hija haipaswi kuendeshwa na nchi moja, bali nchi zote za Kiislamu zinapaswa kushirikishwa katika usimamizi wake."
Mwanazuoni huyo wa Kiislamu amesema hakupaswi kuwepo ubaguzi katika ibada ya Hija na kwamba Waislamu wa nchi zote pasina kuzingatia rangi, lugha au madhehebu wanapaswa kuruhusiwa kuhiji pasina kuwepo vizingiti.
Hivi karibuni, Rais Hassan Rouhani wa Iran alilaani hatua ya Saudia kuwazuia Wairani kutekeleza ibada ya Hija mwaka huu na kusema hatua hiyo ni kwa maslahi ya utawala wa Kizayuni wa Israel.
Kwa upande wake, Waziri wa Utamaduni na Muongozo wa Kiislamu wa Iran amesema njama na vizingiti vya Saudia ni jambo ambalo limewazuia Wairani kutekeleza ibada ya Hija mwaka huu.