Ivory Coast yasisitiza, Uislamu ni dini ya amani
Waziri wa Mambo ya Nje wa Ivory Coast ametilia mkazo udharura wa kupambana na ugaidi na kusema kuwa Uislamu ni dini ya amani na suluhu.
Abdullah Albert Toikeusse Mabri amewaambia mabalozi wa nchi za kigeni mjini Abidjan kwamba Uislamu ni dini ya amani, rehma na upendo na kwamba Ivory Coast inataka kuwepo ushirikiano wa kimataifa kwa ajili ya kung'oa mizizi ya ugaidi.
Mabri amesema kuwa mashambulizi ya kigaidi yanayoshuhudiwa katika maeneo mbalimbali ya dunia hayawezi kukubalika kwa namna yoyote ile na yanapaswa kupigwa vita.
Waziri wa Mambo ya Nje wa Ivory Coast ambaye alikuwa akizungumza katika hafla ya futari ameutaja mwezi wa Ramadhani kuwa ni mwezi wa kutakasa nafsi na kujikurubisha kwa Mwenyezi Mungu na kutoa tena wito wa kuzidishwa mapambano dhidi ya ugaidi.