Apr 17, 2024 06:48 UTC
  • Ebrahim Raisi: Wazayuni wataelewa maana halisi ya majibu ya Iran

Rais wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesema kuwa, iwapo Israel itafanya kosa jingine lolote dhidi ya Iran, basi Wazayuni na waungaji mkono wao wataelewa maana halisi ya majibu ya Jamhuri ya Kiislamu.

Sayyid Ebrahim Raisi alisema hayo jana Jumanne hapa Tehran, wakati aliponana na Sheikh Ali Khatib, Mkuu wa Baraza Kuu la Kiislamu la Waislamu wa Kishia wa Lebanon na kuongeza kuwa, shambulio la Israel kwenye ubalozi wa Iran mjini Damascus Syria ulikuwa ni ushahidi wa kufeli kikamilifu utawala wa Kizayuni katika vita vya Ghaza na kwamba mashambulizi ya kijeshi yaliyofanywa na Iran dhidi ya utawala wa Kizayuni kujibu jinai yake hiyo ilikuwa ni kuitia adabu kidogo tu Israel. Amesema kama utawala huo pandikizi utafanya kosa jingine lolote, hapo Wazayuni na waungaji mkono wao ndipo watakapoona majibu halisi ya Jamhuri ya Kiislamu.

Rais wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran pia amesema kuwa, hivi sasa tena misimamo ya haki ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran imeeleweka vizuri na ubatilifu wa siasa za mapatano na kusalimu amri kunakofanywa baadhi ya nchi za Waislamu pia umeonekana wazi.

Kwa upande wake, Sheikh Ali Khatib, Mkuu wa Baraza Kuu la Kiislamu la Waislamu wa Kishia wa Lebanon amesisitiza kuwa, muqawama wa Lebanon unaunga mkono kikamilifu misimamo ya haki ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran na unajifakharisha nayo kwani ni fakhari kwa umma mzima wa Kiislamu hasa kwa kuzingatia kuwa hakuna nchi yoyote iliyothubutu kuutwanga kwa makombo kiasi chote hiki utawala wa Kizayuni wa Israel isipokuwa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran. 

Tags