Msemaji wa Serikali: Iran kamwe haitoingia kwenye mazungumzo yasiyo na heshima
Msemaji wa serikali ya Rais Masoud Pezeshkian amesema kuwa, Jamhuri ya Kiislamu ya Iran kamwe haitoingia kwenye mazungumzo ambayo yatavunja heshima na itibari yake.
Bi Fateme Mohajerani ameandika hayo kwenye mtandao wa kijamii wa X na huku akisisitizia wajibu wa kuweko mshikamano ndani ya Iran ameandika: Kila mtu anatambua kwamba kamwe Tehran haitokuwa tayari kuingia kwenye mazungumzo yasiyolinda heshima yake.
Aliandika hayo jana Jumamosi kwenye mtandao huo wa X na kusisitiza kuwa, mkakati wa serikali ya Rais Masoud Pezeshkian ni kusikika sauti moja ndani ya Iran.
Amesema, sote tunatambua matatizo yaliyopo. Leo hii tunahitajia zaidi mshikamano na umoja wa kitaifa humu nchini kuliko jana, ili tuweze kuvuka vyema kwenye matatizo.
Pia amesema, mazungumzo baina ya Iran na nchi za Ulaya yataendelea na kila mtu anatambua kuwa mstari mwekundu wa Iran ni itibari na heshima yake.