Iran yaonya: Hujuma za Marekani na Israsel ni tishio kwa amani duniani
https://parstoday.ir/sw/news/iran-i140258-iran_yaonya_hujuma_za_marekani_na_israsel_ni_tishio_kwa_amani_duniani
Iran imeonya kuwa kuendelea kwa hujuma za kijeshi za utawala wa Kizayuni wa Israel huko Gaza, mashambulizi dhidi ya nchi jirani, na upanuzi wa makazi haramu, sambamba na hujuma zisizo halali za Marekani dhidi ya Iran, kunaleta tishio kubwa kwa amani ya kikanda na ya kimataifa huku ikisisitiza tena haki yake ya kujilinda.
(last modified 2026-07-29T14:29:41+00:00 )
Jul 29, 2026 14:28 UTC
  •  Balozi na Naibu Mwakilishi wa Kudumu wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran katika Umoja wa Mataifa, Gholamhossein Darzi,
    Balozi na Naibu Mwakilishi wa Kudumu wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran katika Umoja wa Mataifa, Gholamhossein Darzi,

Iran imeonya kuwa kuendelea kwa hujuma za kijeshi za utawala wa Kizayuni wa Israel huko Gaza, mashambulizi dhidi ya nchi jirani, na upanuzi wa makazi haramu, sambamba na hujuma zisizo halali za Marekani dhidi ya Iran, kunaleta tishio kubwa kwa amani ya kikanda na ya kimataifa huku ikisisitiza tena haki yake ya kujilinda.

Akihutubia Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa, Balozi na Naibu Mwakilishi wa Kudumu wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran katika Umoja wa Mataifa, Gholamhossein Darzi, amesema kuwa licha ya kutangazwa kwa usitishaji mapigano Gaza, utawala wa Kizayuni “unaendelea kukiuka usitishaji huo kwa mashambulizi ya kijeshi yanayoendelea na vikwazo vikali dhidi ya upatikanaji wa misaada ya kibinadamu,” hali inayoongeza ukali wa janga la kibinadamu Gaza.

Mwakilishi wa Iran amesema kuwa kuendelea kwa upanuzi wa makazi ya walowezi wa Kizayuni katika Ukingo wa Magharibi unaokaliwa kwa mabavu, pamoja na vitendo vya mara kwa mara vya uchokozi dhidi ya Lebanon na  Syria, kunazidi kudhoofisha amani na usalama wa kikanda.

Akiashiria Mahakama ya Kimataifa ya Jinai (ICC), mjumbe wa Iran amesema kutolewa kwa hati za kukamatwa dhidi ya Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu tarehe 21 Novemba 2024 ni “ukumbusho wa wazi kwamba hakuna aliye juu ya sheria za kimataifa.” ICC inamsaka Netanyahu na waziri wake wa zamani wa vita Yoav Gallant kutokana na jinai zao huko Gaza.

Darzi aidha ameikosoa vikali Marekani kwa kukiuka Mkataba wa Umoja wa Mataifa na misingi ya msingi ya sheria za kimataifa kupitia mashambulizi dhidi ya miundombinu ya kiraia.

Mjumbe huyo ametaja shambulizi dhidi ya Shule ya Minab kusini mwa Iran kuwa “mfano wa kusikitisha na usiopingika wa uhalifu wa kivita,” akiongeza kuwa maafisa waandamizi wa Marekani waliwahi kukiri hadharani kuhusu mashambulizi hayo.

Amesema: “Wale wanaohusika na uhalifu huu mkubwa, mapema au baadaye, watawajibishwa mbele ya vyombo husika vya kimataifa vya mahakama.”

Akihitimisha, mjumbe huyo amesisitiza kuwa hatua za Iran zinatokana na haki ya kujilinda chini ya sheria za kimataifa.

Amesema: “Iran imetekeleza na itaendelea kutekeleza haki yake ya asili ya kujilinda, kwa mujibu wa Ibara ya 51 ya Mkataba wa Umoja wa Mataifa, ili kuwalinda watu wake na kulinda mamlaka yake, uadilifu wa ardhi yake na maslahi yake muhimu ya kitaifa dhidi ya vitendo vya uchokozi vya Marekani.”