"Zaidi ya asilimia 72 ya wapiga kura kushiriki katika uchaguzi Iran"
https://parstoday.ir/sw/news/iran-i29202-zaidi_ya_asilimia_72_ya_wapiga_kura_kushiriki_katika_uchaguzi_iran
Waziri wa Mambo ya Ndani wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesema kuwa, kwa mujibu wa uchunguzi wa kuaminika wa karibuni kabisa wa maoni, zaidi ya asilimia 72 ya watu waliotimiza masharti ya kupiga kura watashiriki katika uchaguzi wa keshokutwa Ijumaa hapa nchini, na kuna uwezekano idadi hiyo ikaongezeka katika kipindi cha siku hizi chache zilizobakia.
(last modified 2026-01-14T08:12:18+00:00 )
May 17, 2017 03:12 UTC
  • Waziri wa Mambo ya Ndani wa Iran, Abdolreza Rahmani-Fazli
    Waziri wa Mambo ya Ndani wa Iran, Abdolreza Rahmani-Fazli

Waziri wa Mambo ya Ndani wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesema kuwa, kwa mujibu wa uchunguzi wa kuaminika wa karibuni kabisa wa maoni, zaidi ya asilimia 72 ya watu waliotimiza masharti ya kupiga kura watashiriki katika uchaguzi wa keshokutwa Ijumaa hapa nchini, na kuna uwezekano idadi hiyo ikaongezeka katika kipindi cha siku hizi chache zilizobakia.

Uchaguzi wa 12 wa Rais wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran pamoja na uchaguzi wa tano wa mabaraza ya Kiislamu ya miji na vijiji unatarajiwa kufanyika Ijumaa ya Mei 19.

Waziri wa Mambo ya Ndani wa Iran, Abdolreza Rahmani-Fazli, alisema hayo jana usiku katika mahojiano maalumu aliyofanyiwa na Kanali ya Pili ya Televisheni ya Shirika la Sauti na Televisheni la Jamhuri ya Kiislamu ya Iran IRIB na kuongeza kwamba, watu milioni 56 na laki nne na elfu 10 na 234 wametimiza masharti ya kupiga kura nchini Iran. Ameongeza kuwa, karibu maafisa milioni moja na laki tano wanaendesha na kusimamia uchaguzi huo.

Wananchi wa Iran waliotimiza masharti ya kupiga kura, wakubwa kwa wadogo hujitokeza kwa wingi kupiga kura. Kila raia wa Iran aliyebaleghe yaani aliyetimiza miaka 15 ana haki ya kupiga kura humu nchini

 

Amesema, kuna uwezekano mkubwa mshindi wa uchaguzi wa rais akapatikana katika hatua ya kwanza ya uchaguzi huo kutokana na baadhi ya wagombea kujitoa kwenye kinyangányiro hicho kwa maslahi ya wagombea wengine.

Aidha amesema, matokeo ya uchaguzi yatangazwa mara moja na kuongeza kuwa, kwa mujibu wa katiba ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran, waziri wa mambo ya ndani ndiye mwenye haki ya kutangaza matokeo ya mwisho ya kura naye atatangaza matokeo hayo mara yatakapomfikia.