Rais Rouhani: Zama za Marekani kuitawala Iran haziwezi kurejea
https://parstoday.ir/sw/news/iran-i51362-rais_rouhani_zama_za_marekani_kuitawala_iran_haziwezi_kurejea
Rais Hassan Rouhani wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran sambamba na kulaani misimamo ya uhasama ya Marekani kwa Iran tangu ushindi wa Mapinduzi ya Kiislamu miaka 40 iliyopita, amesema zama za Washington kuishurutisha na kuitawala Iran zimekwisha na katu haziwezi kurejea.
(last modified 2026-03-17T04:36:21+00:00 )
Feb 05, 2019 23:44 UTC
  • Rais Rouhani: Zama za Marekani kuitawala Iran haziwezi kurejea

Rais Hassan Rouhani wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran sambamba na kulaani misimamo ya uhasama ya Marekani kwa Iran tangu ushindi wa Mapinduzi ya Kiislamu miaka 40 iliyopita, amesema zama za Washington kuishurutisha na kuitawala Iran zimekwisha na katu haziwezi kurejea.

Rais Rouhani aliyasema hayo jana katika Duru ya 36 ya Tuzo ya Kitabu cha Mwaka na Duru ya 26 ya Tuzo ya Kimataifa ya Vitabu hapa mjini Tehran na kuongeza kuwa, hatua ya Marekani, nchi za Ulaya na baadhi ya nchi vibaraka katika eneo ya kuiwekea nchi hii vikwazo na mzingiro wa kila upande imeshindwa kufikia malengo yaliyotarajiwa, kutokana na kusimama kidete, kuwa na matumaini na kujiamini taifa la Iran. 

Ameashiria hatua ya Marekani ya kuwazuia 'wanasayansi' wake wanne kuja kupokea tuzo zao katika sherehe hizo za jana hapa nchini ikitishia kuwanyima viza za kurejea Marekani, na kusema kuwa kitendo hicho kimebainisha wazi kuwa Wamarekani wenyewe wapo chini ya vikwazo vya serikali yao.

Rais Rouhani akikabidhi tuzo

Rais wa Iran amebainisha kuwa, "Mnatumia lugha ya porojo, isiyo ya kidiplomasia na isiyokubalika. Mnasema mtasalia Iraq ili kuipiga darubini Iran, katika hali ambayo awali mlidai mko katika nchi hiyo eti kupambana na ugaidi."

Rais Hassan Rouhani amesisitiza kuwa, Wairani, Wairaqi na mtu yeyote yule duniani hawezi kukubaliana na fikra hiyo, na kwamba taifa la Iran katu haliwezi kusalimu amri mbele ya matakwa batili ya Marekani na daima itaendelea kuwa katika mkondo wa maendeleo na kujistawisha.