Rais Rouhani atilia mkazo kuimarishwa ushirikiano na nchi mbalimbali za dunia
Rais wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesisitiza ulazima wa kuimarishwa ushirikiano wa kiuchumi, kiutamaduni na kielimu kati ya Iran na nchi mbalimbali za dunia.
Rais Hassan Rouhani leo Jumanne amekutana na kufanya mazungumzo na mabalozi wapya 13 wa Iran katika nchi tofauti duniani kabla ya kuelekea katika vituo vyao vya kazi na kuwataka mabalozi hao kuarifisha na kutangaza uwezo wa Iran kwa wawekezaji, sekta binafsi na serikali za nchi wanakokwenda. Rais Rouhani amewatolea wito mabalozi hao wapya kufanya juhudi zaidi za kustawisha na kuimarisha uhusiano na ushirikiano wa pande zote na nchi nyingine.

Mabalozi wapya 13 wa Iran walioteuliwa katika nchi za Ubelgiji, Sweden, Norway, Denmark, Beralus, Armenia, Serbia, Afrika Kusini, Nigeria, Qirqizistan, Srilanka, Mauritania na Croatia pia wametoa ripoti kuhusu hali ya mahusiano katika nyanja mbalimbali kati ya Iran na nchi wanakokwenda kuhudumu na kusisitiza kuwa watafanya kazi kwa bidii na umakini ili kustawisha uhusiano wa kiuchumi na ushirikiano wa pande zote kati ya Iran na nchi nyingine.