Mousavi: Wairani hawatawasahau marafiki zao katika kipindi hiki kigumu
https://parstoday.ir/sw/news/iran-i59742-mousavi_wairani_hawatawasahau_marafiki_zao_katika_kipindi_hiki_kigumu
Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran amezishukuru nchi zinazoendelea kutuma misaada hapa nchini kwa ajili ya kukabiliana na maambukizi ya virusi vya Corona na kusema serikali na wananchi wa Iran kamwe hawatawasahau maraiki zao katika kipindi hiki kigumu.
(last modified 2023-11-27T08:44:11+00:00 )
Mar 14, 2020 10:32 UTC
  • Mousavi: Wairani hawatawasahau marafiki zao katika kipindi hiki kigumu

Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran amezishukuru nchi zinazoendelea kutuma misaada hapa nchini kwa ajili ya kukabiliana na maambukizi ya virusi vya Corona na kusema serikali na wananchi wa Iran kamwe hawatawasahau maraiki zao katika kipindi hiki kigumu.

Katika ukurasa wake wa Twitter, Sayyid Abbas Mousavi ameashiria mawasiliano ya simu na jumbe za Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran, Muhammad Javad Zarif na jitihada zinazofanywa na balozi wa Jamhuri ya Kiislamu nje ya nchi na kusema: Mbali na nchi za China, Uturuki, Imarati, Ujerumani, Ufaransa na Uingereza, Tehran imepokea misaada ya kifedha, zana na vifaa vya tiba kutoka nchi za Japan, Qatar, Jamhuri ya Azerbaijan na Russia. 

Itakumbukwa kuwa Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran Alkhamisi iliyopita alimwandikia barua Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, Antonio Guterres akisema: Licha ya uwezo mkubwa wa kielimu na kisayansi wa mfumo wa afya wa Iran wa kuweza kukabiliana na virusi vya Corona, lakini vikwazo na masharti ya Marekani yanayozuia kuuzwa dawa na vifaa vya tiba kwa Iran vinakwamisha mapambano ya Jamhuri ya Kiislamu katika kukabiliana maambukizi ya virusi hivyo. 

Katika barua hiyo Muhammad Javad Zarif amesisitiza udharura wa kuondolewa vikwazo vyote vya upande mmoja na vya kidhalimu vya Marekani dhidi ya Iran. 

Muhammad Javad Zarif

Hadi sasa karibu watu laki moja na 46 wameambukizwa virusi vya Corona katika nchi mbalimbali za dunia na zaidi ya elfu 75 wamepona janga hilo. Wagonjwa wasiopungua 5,400 wameaga duniani. 

Sambamba na hayo Wizara ya Afya ya Iran imetangaza kuwa, hadi sasa wagojwa 4,339 wa Corona wametibiwa na kupona hapa nchini na kuruhusiwa kurudi nyumbani.

Mkuu wa Idara ya Mawasiliano ya Umma ya Wizara ya Afya ya Iran, Dokta Kianoush Jahanpour amesema kuwa, zaidi ya watu elfu 12 wameambukizwa virusi vy Corona hapa nchini na kwamba inasikitisha kuwa 611 miongoni mwao wameaga dunia kutokana na ugonjwa huo.

Sambamba na hayo serikali na vikosi vya jeshi vinaendelea kupambana na maambukizi ya virusi hivyo kwa kutoa huduma za haraka za kupima, kuwafuatilia watu waliowasiliana na waathirika wa Corona, kutenganisha na kuwaweka karantini na kutoa matiba kwa kushirikiana na matabaka yote ya wananchi.