Mjumuiko mkubwa wa Siku ya Kimataifa ya Quds kufanyika katika intaneti
Kutokana na kuenea janga la COVID-19 au corona kote duniani na vizingiti vilivyowekwa katika kuandaa mijimuiko ya watu mitaani au katika kumbi, sasa kutafanyika mjumuiko mkubwa wa waungaji mkono wa Palestina katika intaneti.
Kwa mujibu wa Shirika Rasmi la Habari la Iran, IRNA, wananchi wanamapinduzi wa Iran na wapigania uhuru kote duniani wanaitembelea www.qudsday.net ili kushiriki katika mjumuiko mkubwa wa waungaji mkono wa Palestina. Mjumuiko huo wa intaneti utawaleta pamoja watu wa mataifa mbali mbali ya dunia kwa lengo la kuadhimisha Siku ya Kimataifa ya Quds.

Inafaa kuashiria hapa kuwa, Mwasisi wa Jamhuri ya Kiislamu hayati Imam Khomeini (Mwenyezi Mungu amrehemu) ndiye aliyeipa siku hiyo ya Ijumaa ya mwisho ya mwezi Ramadhani jina la Siku ya Kimataifa ya Quds kwa shabaha ya kuakisi dhulma ya kihistoria inayofanywa na Israel, kwa himaya ya madola ya Magharibi yanayodai kutetea haki za binadamu, dhidi ya watu wanaoendelea kudhulumiwa na kukandamizwa wa Palestina na ardhi yao takatifu. Tokea ushindi wa Mapinduzi ya Kiislamu ya Iran mwaka 1979, Siku ya Kimataifa ya Quds imekuwa ikiadhimishwa kupitia maandamano na makongamano kote duniani.
Kesho Ijumaa 22 Mei 2020 sawa na tarehe 28 Ramadhani 1441 itakuwa Siku ya Kimataifa ya Quds .