Mousavi: Moto wa karibuni nchini Iran hauhusiani na hujuma za kimtandao
Akijibu madai kuhjusu uharibifu na hujuma za kimtandao dhidi ya Iran, Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran amesema kuwa, moto uliotokea hivi karibuni hapa nchini hausiani kivyovyote na hujuma za kimtandao.
Akizungumza na waandishi habari kuhusu madai ya kujiri uharibifu na hujuma za kimtandao dhidi ya Iran kulikofanywa na baadhi ya serikali na tawala, Sayyid Abbas Mousavi ameongeza kuwa maelfu ya hujuma za kimtandao zinajiri kila siku katika miundombinu ya Iran jambo ambalo si jipya; na nyingi ya hujuma hizo zinazuiwa na kusambaratishwa na mifunzo ya ulinzi na timu za kompyuta za kukabiliana na matukio mbalimbali bila ya kuacha athari yoyote.
Mousavi ameashiria namna moto wa hivi karibuni usivyohusiana na hujuma zozote za kimtandao na pia agizo la Rais wa Marekani la kutekelezwa hujuma za kimtandao dhidi ya Iran na nchi nyingine na kueleza kuwa: Kuanzia sasa mshukiwa mkuu wa hujuma yoyote ya kimtandao dhidi ya Iran itakuwa ni serikali ya Marekani labda ithibitike kinyume chake.
Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya Iran amesema kuwa, Tehran italiweka katika ajenda yake ya kazi suala la kufuatilia kimataifa agizo hilo lililo kinyume cha sheria na la kihalifu na kuthibitisha kuhusika Marekani. Amesisitiza kuwa, Iran ina haki ya kuchukua hatua munasibu katika wakati mwafaka.