Sep 04, 2020 12:05 UTC

Jumuiya ya Walimu wa Chuo Kikuu cha Kidini (Hawza) cha Qum hapa Iran imelaani vikali kuvunjiwa heshima matukufu ya Qur'ani Tukufu na Mtume Muhammad SAW na kusisitiza kuwa, kuivunjia heshima Qur'ani Tukufu kwa kisingizio cha uhuru wa itikadi kwa hakika ni kuukata roho uhuru huo na kungamiza kijinai, itakadi ya watu.

Ijumaa iliyopita ya tarehe 28 Agosti, 2020, maadui wa Uislamu walifanya maandamano haramu katika mji wa Malmö wa kusini mwa Sweden na kuchoma moto nakala moja ya Qur'ani Tukufu.

Si hayo tu, lakini pia gazeti la maadui wa Uislamu la Charlie Hebdo la nchini Ufaransa, siku ya Jumanne lilifanya utovu wa adabu mpya wa kuchora vibonzo vya kumvunjia heshima Mtume Muhammad SAW.

Jumuiya ya Walimu  wa Chuo Kikuu cha Kidini (Hawza) cha Qum hapa Iran imetoa tamko kali leo Ijumaa na kusisitiza kuwa, kitendo cha kiuadui na cha kuogofya cha kuvunjia heshima matukufu ya Qur'ani Tukufu huko Sweden ni jinai kubwa ambayo haipaswi kusamehewa.

Kitabu Kitakatifu cha Qur'ani kinachowachoma nyoyo maadui wa Uislamu

 

Taarifa hiyo imeongeza kuwa, siasa za kiuadui zinazoendeshwa na Uzayuni wa kimataifa na uistikbari wa dunia zinapangwa katika taasisi na mashirika ya Kizayuni ya Marekani na baadhi ya nchi za Ulaya na baadaye kupewa vitimbakwiri watenda jinai kuzitekeleza.

Taarifa hiyo imeongeza kuwa, vitendo vya kiwendawazimu vya kuchochea hisia za Waislamu vimetokana na fikra ya Kimarekani ya kukabiliana na kudhihiri ustaarabu wa Kiislamu na kusambaratika mfumo wa Kimarekani unaotawala duniani leo.

Jumuiya ya Walimu  wa Chuo Kikuu cha Kidini (Hawza) cha Qum hapa Iran pia imesema kwenye taarifa yake hiyo kwamba, taasisi na mashirika ya kimataifa ya kutetea haki za binadamu yanapaswa kuchukua hatua kali za kukabiliana na uadui wa kuvunjiwa heshima matukufu ya Kiislamu unaofanywa kwa malengo maalumu ya kibeberu.

Tags