Raisi: Adui amekasirishwa na hatua za Iran za kusambaratisha vikwazo
-
Rais Sayyid Ebrahim Raisi
Rais wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ameyataja machafuko na vikwazo vya nchi za Magharibi kuwa ni pande mbili za sarafu moja na kueleza kuwa, adui amekasirishwa na hatua zinazochukuliwa na serikali na wananchi wa Iran kwa ajili ya kusambaratisha vikwazo hivyo.
Rais Sayyid Ebrahim Raisi wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ambaye alikuwa akizungumza mubashara na wananchi kupitia televisheni ya taifa ameashiria kuwadia sherehe za "Alfajiri Kumi" za kuadhimisha ushindi wa Mapinduzii ya Kiislamu hapa nchini na kueleza kuwa, moja ya sababu zilizopelekea kuibuka ghasia na machafuko hivi karibuni hapa nchini ni kwamba, adui alitambua kuwa vikwazo vyake havijakuwa na taathira kutokana na hatua zinazochukuliwa na serikali na kusimama imara wananchi wa Iran.
Raisi amese kuwa, kati ya sababu zilizomfanya adui aikasirikie serikali na wananchi wa Iran ni kuongezeka mauzo ya mafuta ya taifa, kukua uzalishaji kwa silimia tano, kupatikana ajira mpya karibu milioni moja na kupungua mfumuko wa bei.
Rais wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ameongeza kuwa, adui alianzisha njama kutokana na kukua kwa vielezi vya uchumi wa nchi hii na kwamba, kwa irada na utendaji wa serikali, na vilevile kwa kutegemea uwezo na suhula nyingi zilizopo nchini, harakati hii itashika kasi na kuimarika zaidi siku baada ya siku.
Rais Ebrahim Raisi pia amezitaka nchi za Ulaya ziachane na misimamo na vigezo vyao vya kinafiki na kindumakuwili.