Al Jaafari: Israel na ugaidi ni pande mbili za sarafu moja
Mwakilishi wa kudumu wa Syria katika Umoja wa Mataifa amesisitiza kuwa, utawala wa Kizayuni wa Israel na ugaidi ni pande mbili za sarafu moja na amemlaumu vikali Nikolay Mladenov, mratibu maalumu wa umoja huyo katika mazungumzo ya mapatano ya Mashariki ya Kati kwa kudharau kutaja milima ya Golan ya Syria inayokaliwa kwa mabavu na Israel, katika ripoti yake kwa umoja huo.
Bashar al Jaafari alisema hayo jana usiku katika kikao cha Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kilichoitishwa kwa ajili ya kuzungumzia masuala ya Mashariki ya Kati.
Amesema, afisa huyo wa Umoja wa Mataifa amelidharau suala la milima ya Golan ya Syria inayokaliwa kwa mabavu na Israel katika hali ambayo suala hilo ni moja ya masuala muhimu sana ya Mashariki ya Kati.
Ameongeza kuwa, Syria itaendelea kuwa na msimamo wake usiotetereka wa kuwaunga mkono wananchi wa Palestina, kuunga mkono haki yao ya kujiamulia wenyewe masuala yao, kuundwa nchi moja yenye nguvu na utulivu katika ardhi yote ya Palestina na pia kutekelezwa kivitendo haki ya wakimbizi wa Palestina ya kurejea kwenye ardhi zao za jadi.
Mwakilishi maalumu wa Syria katika Umoja wa Mataifa aidha amesema, kitendo cha Baraza la Usalama cha kuendelea kupuuza jinai zinazofanywa na Israel ndiko kunakozidisha kiburi cha utawala huo dhalimu. Amesema, upuuzaji huo umezidisha kiburi cha utawala wa Kizayuni kiasi kwamba hivi sasa unaunga mkono waziwazi magenge ya kigaidi bila ya woga wowote.