Jul 12, 2018 14:59 UTC
  • Saudi Arabia yamtia nguvuni mwanazuoni wa nchi hiyo kwa kukosoa serikali

Utawala wa Saudi Arabia umemtia nguvuni mwanazuoni wa kidini wa nchi hiyo baada ya kukosoa siasa za utawala wa kifalme wa nchi hiyo na Marekani.

Askari usalama wa Saudi Arabia leo Alkhamisi wamevamia nyumba ya Sheikh Safar bin Abdul-Rahman al-Hawali mjini Makka na kumtia nguvuni na kisha wakampeleka kusikojulikana akiwa pamoja na mtoto wake mmoja wa kiume. 

Sheikh Safar Al-Hawali ametiwa nguvuni baada ya kuchapisha kitabu alichokipa jina la "Waislamu na Ustaarabu wa Kimagharibi". Ndani ya kitabu hicho msomi huyo ameikosia vikali serikali ya Saudi Arabia kutokana na fedha inazotoa kwa serikali ya Marekani na mabilioni ya dola iyoyatoa kwa Rais Donald Trump wa Marekani wakati wa safari yake mjini Riyadh. 

Kitabu hicho cha msomi wa Saudi Arabia pia kimeitaja Imarati kuwa inatekeleza siasa na sera za Mayahudi katika eneo la Mashariki ya Kati. Sheikh al Hawali  ameandika kuwa: Hakuna mtu anayeshuku kuwa Rais Abdul Fattah al Sisi wa Misri, Mahmoud Abbas wa Mamlaka ya Ndani ya Palestina na watawala wengine wengi wa nchi za Kiarabu ni dhalili na vibaraka wa Marekani.

Katika mwaka mmoja uliopita hususan baada ya kuteuliwa Muhammad bin Salman kuwa mrithi wa kiti cha ufalme wa Saudi Arabia, makumi ya wafanyabiashara, wanazuoni wa dini, wasomi na hata wanamfalme wa nchi hiyo wamekamatwa na kufungwa jela

Tags