Ndege za kivita za Saudia zaua watu 15 Hudaydah, Yemen
Watu wasiopungua 15 wamepoteza maisha kufuatia hujuma ya ndege za kivita za Saudia katika barabara ya kistratijia inayounganisha mji mkuu wa Yemen, Sana'a na mji wa bandarini wa Hudaydah magharibi mwa nchi hiyo.
Televisheni ya Al Masirah inayofungamana na Harakati ya Ansarullah imeripoti kuwa zaidi ya watu 20 wamejeruhiwa katika hujuma hiyo iliyojiri katika barabara inayojulikana kama Kilo 16.
Hayo yamejiri wakati ambao Mpango wa Chakula Duniani wa Umoja wa Mataifa (WFP) umetahadharisha kuhusiana na baa la njaa linaloikabili nchi ya Yemen na kutoa wito wa kusaidiwa nchi hiyo. WFP imesema, mashambulio ya anga ya Saudi Arabia na washirika wake dhidi ya Bandari ya Al-Hudaydah yamekuwa yakiwalenga wafanyakazi wa mashirika ya misaada ya kibinadamu pamoja na miundombinu ya mashirika hayo na hivyo kukwamisha kabisa juhudi za kuwafikishia misaada ya chakula wananchi wa Yemen wanaokabiliwa na uhaba mkubwa wa chakula.
Saudi Arabia ikisaidiwa na Marekani, Israel, Imarati na nchi nyingine kadhaa iliivamia Yemen mwezi Machi mwaka 2015 na hadi sasa raia zaidi ya 15,000 wasio na hatia, hasa watoto na wanawake wa nchi hiyo wameuawa na mamilioni ya wengine wamelazimika kuwa wakimbizi ndani na nje ya nchi.