Makumi ya Wayemeni waaga dunia kwa ugonjwa wa dondakoo (Diptheria)
Wizara ya Afya ya Yemen imetangaza kuwa tangu mwaka mmoja uliopita hadi sasa watu 141 wameaga dunia kwa ugonjwa wa dondakoo; wengi wakiwa ni watoto wadogo.
Wizara ya Afya ya Yemen imetangaza kuwa zaidi ya watu 2570 wameambukizwa ugonjwa wa dondakoo nchini humo hadi kufikia sasa. Taarfa ya wizara hiyo imeongeza kuwa vita ni chanzo kikuu cha kuenea maradhi ya kipindupindu na dondakoo huko Yemen; vita vilivyoanzishwa dhidi ya raia wa Yemen na muungano vamizi unaoongozwa na Saudia.
Shirika la Afya Duniani (WHO) lilitangaza kabla ya kutolewa taarifa ya Wizara ya Afya ya Yemen kwamba karibu raia wa nchi hiyo milioni 16 wanahitaji misaada na huduma za kiafya. Wakati huo huo WHO imeripoti kuwa mamia ya watu wengine pia wamebainika kuambukizwa ugonjwa wa dondakoo katika mikoa 15 kati ya 22 ya Yemen; ambapo makumi ya raia walioambukizwa ugonjwa huo huishia kupoteza maisha.
Kwa mujibu wa ripoti hiyo ya Shirika la Afya Duniani; karibu asilimia 80 ya jamii ya wananchi wa Yemen wanataabika na matatizo mbalimbali kama uhaba wa chakula, maji safi na salama na huduma za matibabu.