Sheikh Issa Qassim alaani mpango wa kukaribishwa Wazayuni Bahrain
Mwanazuoni maarufu wa Kiislamu nchini Bahrain, Sheikh Isa Qassim amekosoa vikali hatua ya kualikwa Wazayuni kwenye Kongamano la Kibiashara linalotazamiwa kufanyika katikati ya mwezi huu wa Aprili nchini humo.
Kiongozi huyo wa kidini amesema kitendo hicho cha kuwakaribisha nchini Bahrain Wazayuni ni hatua moja kuelekea katika njia ya kujidhalilisha adui mkubwa zaidi kwa ulimwengu wa Kiislamu.
Ayatullah Sheikh Issa Qassim amesema hatua hiyo sio tu ni kujidhalilisha na kujipendekeza kwa maadui, bali pia ni kitendo cha kujitweza, fedheha na aibu kubwa.
Mwanazuoni huyo maarufu wa Kiislamu nchini Bahrain amesisitiza kuwa, utawala wa Kizayuni wa Israel ndiye adui nambari moja wa ulmwengu wa Kiislamu ambaye hapaswi kukaribishwa, kupokewa wala kupewa mkono.
Kabla ya hapo, Wabunge wa Bahrain walitoa taarifa ya pamoja inayopinga kukaribishwa nchini humo viongozi hao wa Kizayuni. Taarifa hiyo imebainisha kuwa, "Bunge linasisitizia uungaji mkono wake kwa kadhia ya wananchi wa Palestina, na hilo litasalia kuwa kipaumbele kwa Wabahrain na Waarabu wote."
Bahrain kama aghalabu ya nchi za Kiarabu haina uhusiano wa kidiplomasia na utawala haramu wa Israel.
Waisraeli wanne ni miongoni mwa makumi ya watu walioalikwa kuzungumza katika mkutano huo wa wawekezaji unaotazamiwa kufanyika mjini Manama kati ya Aprili 15 na 18.