Hania: Wananchi wa Palestina hawataruhusu kutekelezwa mipango ya adui huko Quds
Mkuu wa Ofisi ya Kisiasa ya Harakati ya Mapambano ya Kiislamu ya Palestina (Hamas) amesema kuwa mipango ya adui Mzayuni ya kuugawa msikiti wa al Aqsa itagonga mwamba na kusisitiza kuwa wananchi wa Palestina hawataruhusu kutekelezwa mipango ya adui na kubadilishwa athari na nembo za mji wa Quds.
Ismail Hania amesisitiza kuwa kuna udharura wa kukabiliana kwa dhati na kwa ushujaa na mipango ya adui Mzayuni na kueleza kuwa: Matukio yanayojiri katika eneo kivyovyote vile hayawezi kulisahaulisha suala la Palestina kwa sababu Quds itaendelea kuwa kituo cha mapambano na makabiliano dhidi ya adui Mzayuni.
Hania ameongeza kusema kuwa, utawala wa Kizayuni inastafidi na matukio na vita vya ndani katika baadhi ya nchi za eneo hili ili kusogeza mbele na kutekeleza njama zake hatari dhidi ya msikiti wa al Aqsa; lakini wananchi wa Palestina wataendelea kuutetea na kuilinda Quds na matukufu ya Kiislamu.
Mkuu wa Ofisi ya Kisiasa ya Hamas aidha amezitolea wito pande tatu za Palestina, Kiarabu na Kimataifa kuchukua hatua za kukabiliana na mpango wa utawala wa Kizayuni wa kuuyahudisha msikiti wa al Aqsa. Hania amezitolea wito pia nchi na wapigania uhuru wote duniani kuususia utawala wa Kizayuni na kuutenga ili uache mipango yake michafu dhidi ya msikiti huo mtakatifu.