Uturuki yasema imemtia mbaroni dadake Abu Bakr Baghdadi
https://parstoday.ir/sw/news/west_asia-i57068-uturuki_yasema_imemtia_mbaroni_dadake_abu_bakr_baghdadi
Uturuki imetangaza habari ya kumtia mbaroni dada ya Abu Bakr al-Baghdadi, kinara wa kundi la kigaidi la Daesh (ISIS) aliyejiua katika operesheni ya Marekani hivi karibuni.
(last modified 2023-11-27T08:44:11+00:00 )
Nov 05, 2019 03:57 UTC
  • Uturuki yasema imemtia mbaroni dadake Abu Bakr Baghdadi

Uturuki imetangaza habari ya kumtia mbaroni dada ya Abu Bakr al-Baghdadi, kinara wa kundi la kigaidi la Daesh (ISIS) aliyejiua katika operesheni ya Marekani hivi karibuni.

Mkurugenzi wa Mawasiliano katika Ofisi ya Rais wa Uturuki, Fahrettin Altun amesema Rasmiya Awad, mwenye umri wa miaka 65 alikamatwa jana Jumamtatu katika operesheni ya jeshi la Uturuki karibu na mji wa Azaz, mkoani Halab kaskazini mwa Syria.

Amesema vyombo vya intelijensia vya Uturuki vinatazamiwa kumhoji Rasmiya Awad pamoja na mume wake ambaye pia alikamatwa katika operesheni hiyo, kuhusu mikakati na utendaji kazi wa ISIS.

Aidha watoto watano waliokuwa pamoja na dada yake Baghdadi wanazuilia na vyombo vya usalama nya Uturuki, ili kujua iwapo wana uhusiano au walikuwa mateka.

 Abu Bakr al-Baghdadi, kinara wa ISIS aliyeuawa

Mkurugenzi wa Mawasiliano katika Ofisi ya Rais wa Uturuki, amesema kukamatwa ndugu wa kike wa Baghdadi kunaonesha azma na irada ya Uturuki ya kupambana na magenge ya kigaidi.

Jumapili ya wiki iliyopita Rais Donald Trump wa Marekani alitangaza kwamba kinara huyo wa Daesh (ISIS) Abu Bakr al-Baghdadi aliuawa katika operesheni maalumu iliyofanywa na askari wa nchi hiyo huko katika mkoa wa Idlib, nchini Syria. Trump amekuwa akisisitiza kuwa, serikali iliyopita ya Barack Obama ya nchi hiyo ndiyo iliyoasisi genge la kigaidi la Daesh.