Kuporomoka vibaya Benjamin Netanyahu na chama chake cha Likud
-
Benjamin Netanyahu
Matokeo ya uchunguzi mpya wa maoni huko Israel (Palestina inayokaliwa kwa mabavu) yanaonyesha kuwa, uungaji mkono wa wananchi kwa chama cha Likud kinachoongozwa na Waziri Mkuu Benjamin Netanyahu unaendelea kupungua kwa kasi siku baada ya siku.
Mtandao wa gazeti la Jerusalem Post umeandika, uchunguzi wa maoni uliotangazwa na Radio ya Israel unaonyesha kuwa, katika kipindi cha miezi miwili iliyopita, chama cha Likud kimepoteza viti 10 na hivyo kuzidi kuporomoka.
Ripoti zinasema kuwa, mpromoko huo wa Netanyahu na chama chake cha Likud umetokana na serikali ya sasa ya Waziri Mkuu huyo kushindwa kuzipatia ufumbuzi changamozoto zinazoukabili utawala huo ghasibu kama virusi vya corona na kudorora uchumi.
Wakati Netanyahu na chama chake cha Likud wakiporomoka, hasimu wao yaani chama cha Bluu na Nyeupe kinachoongozwa na Waziri wa Vita Benny Gantz kinazidi kupata umashuhuri na uungaji mkono na hivyo kutishia mustakabali wa kisiasa wa Netanyahu.
Matokeo ya uchunguzi huo yanatangazwa katika hali ambayo katika wiki za hivi karibuni, ardhi zinazokaliwa kwa mabavu (Israel) zimekuwa zikishuhudia maandamano makubwa dhidi ya baraza la mawaziri la Waziri Mkuu Benjamin Netanyahu. Maandamano hayo yametokana na utendaji mbovu wa Netanyahu katika kukabiliana na janga la corona katika ardhi zinazokaliwa kwa mabavu sambamba na kuongezeka matatizo ya kiuchumi.
Aidha wauguzi na wafanyakazi wa sekta ya afya huko Israel wiki iliyopita walianza mgomo wakilalamikia uchache wa wafanyakazi na uhaba wa vitendea kazi hali ambayo inawafanya wafanye kazi katika mazingira magumu na hatari hasa katika kipind hiki cha kuenea virusi vya Corona.