Bomoa bomoa ya Wazayuni yawaacha Wapalestina 800 bila makazi
Shirika moja la kiraia limeripoti kuwa, mamia ya wananchi wa Palestina wameachwa bila makazi kutokana na bomoa bomoa ya utawala wa Kizayuni wa Israel.
Taarifa ya shirika la B’Tselem imesema kuwa, Wapalestina zaidi ya 800 katika Ukingo wa Magharibi wa Mto Jordan wameachwa bila makazi baada ya nyumba zao kubomolewa na utawala haramu wa Israel tokea mwanzoni mwa mwaka huu hadi sasa.
Taarifa hiyo imebainisha kuwa, hii ndiyo idadi kubwa ya Wapalestina kuachwa bila makazi kutokana na sera hiyo ya ubomozi ya Israel tokea mwaka 2016, ambapo Wapalestina 1,500 waliachwa bila makazi baada ya nyumba zao kubomolewa.
Ripoti ya B’Tselem imetolewa muda mfupi baada ya jeshi katili la Israel kubomoa nyumba za Wapalestina 80 wa Kibedui katika Ufukwe wa Magharibi.
Siku ya Jumanne, mabuldoza ya utawala huo ghasibu yalibomoa kikamilifu kijiji kizima cha Humsa al-Buqai’a, cha Mabedui wa Kipalestina huko kaskazini mwa Bonde la Jordan.
Hivi karibuni, Harakati ya Mapambano ya Kiislamu ya Palestina (Hamas) ilisisitiza kuwa, utawala wa Kizayuni unabomoa nyumba za wananchi wa Palestinana hivyo inatekeleza kivitendo mpango wake wa kuikalia kwa mabavu sehemu kubwa ya ardhi ya Ukingo wa Magharibi wa Mto Jordan.