Jul 28, 2023 14:45 UTC
  • Mamilioni ya wafuasi wa Ahlulbait washiriki maombolezo ya Imam Hussein (AS) Siku ya Ashura

Mamilioni ya Waislamu katika Jamhuri ya Kiislamu ya Iran na maeneo mengine ya dunia leo wameshiriki shughuli ya siku ya Ashura ya kukumbuka siku ya kuuliwa shahidi mjukuu wa Mtume Muhammad (SAW), Imam Hussein bin Ali bin Abi Twalib (AS).

Ashura ni mwezi 10 Mfunguo Nne, Muharram, ambayo mwaka huu imesadifiana na leo Ijumaa tarehe 28 Julai, 2023.

Imam Husain AS aliuawa shahidi kikatili na kinyama mwaka wa 61 Hijria katika jangwa la Karbala nchini Iraq akiwa na umri wa miaka 57 baada ya kuongoza mapambano ya kishujaa ya ushindi wa damu mbele ya upanga.

Mtume Muhammad SAW alitabiriwa na Malaika Jibril ukatili huo aliofanyiwa mjukuu wake katika jangwa la Karbala, tangu enzi za uhai wake na alikuwa wa kwanza kumlilia mjukuu wake huyo kipenzi baada ya kuletewa mchanga na Malaika Jibril, wa eneo ambalo Imam Hussein AS angeliuliwa shahidi.

Kwa kufuata sira na mwenendo huo wa Bwana Mtume Muhammad (SAW), wafuasi wa Ahlulbait na wapenzi wa haki na uadilifu, wamekusanyiika leo katika maeneo mbalimbali ya dunia, kukumbuka kwa huzuni na majonzi jinai hiyo kubwa waliyofanyiwa Watu wa Nyumba Tukufu ya Mtume Muhammad (SAW).

Waombolezaji hapa nchini Iran wakiwa wamevalia nguo nyeusi, kama ishara ya huzuni na majonzi, walikuwa wakibubujikwa na machozi kwa kukumbuka dhulma iliyofanywa na madhalimu dhidi ya kizazi bora cha Mtume Muhammad (saw).

Wairani wanaoshiriki katika maombolezo ya Siku ya Ashura husikiliza hotuba na mashairi kuhusiana na masaibu yaliyomkumba Imam Hussein AS huko Karbala. 

Waislamu wa Nigeria katika maombolezo ya Ashura

Mapambano ya Karbla ya Imam Husain AS na wafuasi wake watiifu yalitokea mwaka 680 AD, na watukufu hao walipigana kishujaa katika vita vya kidhulma dhidi ya maelfu ya wanajeshi wa khalifa wa Bani Umayyah, Yazid mwana wa Muawiya, mwana wa Abu Sufyan ambaye alikuwa adui mkubwa wa Mtume Muhammad (saw) na Waislamu. 

Idhaa ya Kiswahili Sauti ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran inatoa mkono wa pole kwa Waislamu wote na kwa kila mpenda haki na ukombozi duniani kwa mnasaba wa kukumbuka msiba huu mkubwa uliomfika Bwana Mtume Muhammad SAW na Uislamu kiujumla.

Tags