Apr 16, 2024 02:14 UTC
  • Ramaphosa: Kama Israel haitodhibitiwa, vita vya Ghaza vinaweza kuenea ukanda mzima

Rais wa Afrika Kusini kwa mara nyingine ameonya kuhusu hatari ya vita vya Ghaza na kuendelea jinai za utawala wa Kizayuni dhidi ya watu wasio na hatia akisisitiza kuwa kama Israel haitodhibitiwa, basi vita hivyo vinaweza kuenea katika nchi zote za eneo hili.

Rais Cyril Ramaphosa amesema hayo mbele ya waandishi wa habari na kuongeza kuwa, nchi yake tangu awali ilikuwa imeonya kwamba ikiwa mashambulizi ya Israel dhidi ya Wapalestina hayatodhibitiwa na kushughulikiwa kwa uangalifu na hekima kubwa, yanaweza kuzusha vita vikubwa vya ukanda mzima.

Rais Ramaphosa amesema: "Tulionya mapema sana kwamba ikiwa changamoto na vita kati ya Israel na Palestina huko Ghaza havitashughulikiwa kwa uangalifu na busara kubwa ili kuhakikisha kuwa kuna usitishaji wa mapigano na kuruhusiwa kuingia Ghaza misaada ya kibinadamu, basi karibuni hivi vita vitaongezeka na kutoka nje ya mipaka ya utawala wa Kizayuni. 

Jumamosi usiku, Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu ya Iran (SEPAH) lilirusha msururu wa ndege zisizo na rubani na makombora kuutia adabu utawala wa Kizayuni baada ya Israel kushambulia ubalozi mdogo wa Iran mjini Damascus, Syria na kuua maafisa kadhaa wakuu wa jeshi la Iran.

Ramaphosa ametoa mwito kwa pande zote kuwa wavumilivu na kuhakikisha hazizidishi utata kwenye hali tete iliyopo hivi sasa Asia Magharibi. 

Amesema, inabidi mashambulizi ya Israel huko Ghaza yakombeshwe kwani hatupaswi kuwa na migogoro ya kikanda wakati tunajua chanzo cha migogoro hiyo ni nini.