Waislamu Marekani waanzisha kampeni dhidi ya Trump
Waislamu wa Marekani wameanzisha "Harakati ya Kura Milioni Moja" kwa shabaha ya kukabiliana na misimamo inayopiga vita Uislamu ya mgombea urais wa nchi hiyo kwa tiketi ya chama cha Republican, Donald Trump.
Mkurugenzi Mtendaji wa Baraza la Uhusiano wa Uislamu na Marekani (CAIR) Nihad Awad amesema kuwa harakati hiyo ilianza mwaka jana na kwamba ni sehemu ya juhudi za Waislamu wa Marekani za kupambana na propaganda chafu na chuki dhidi ya Uislamu.
Nihad Awad ameongeza kuwa, tangu mwezi Novemba mwaka jana hadi sasa Waislamu laki tatu wamekwishajiunga na harakati hiyo. Vilevile maimamu wa Swala za Jamaa kote nchini Marekani wametakiwa kuhamasisha Waislamu kujiandikisha katika harakati hiyo.
Katika miezi ya hivi karibuni Donald Trump amekuwa akitoa matamshi ya kichochezi dhidi ya Uislamu na Waislamu. Disemba mwaka jana alitoa wito wa kuzuiwa Waislamu kuingia katika ardhi ya Marekani.
Kuna Waislamu karibu milioni tatu na laki tatu nchini Marekani na watayarishaji wa "Harakati ya Kura Milioni Moja" wanasema, kura za Waislamu zinaweza kuwa na taathira kubwa katika majimbo kama Virginia na Florida katika uchaguzi ujao wa rais.
Uchaguzi wa rais nchini Marekani umepangwa kufanyika mwezi Novemba mwaka huu.