Peskov: Itachukua muda kuboresha uhusiano wa Russia na Marekani
Dmitry Peskov Msemaji wa ikulu ya Russia (Kremlin) ametangaza kuwa itachukua muda ili kuimarika uhusiano kati ya Russia na Marekani kutokana na kuharibika pakubwa kwa uhusiano kati ya nchi mbili.
Dmitry Peskov leo Jumatano ameliambia shirika la habari la Tass kwamba: Uhusiano wa Moscow na Washington uliingia dosari kubwa wakati wa utawala wa Rais wa zamani wa Marekani Joe Biden.
Peskov ameongeza kuwa: Bila shaka, kuna udhaifu katika mchakato huu. Itachukua muda kutekeleza jitihada ili kurejesha uhusiano wa nchi mbili katika hali ya kawaida.
Kwa mujibu wa shirika la habari la Tass, hii ni mara ya kwanza katika historia za zama hizi ambapo miezi sita imepita tangu rais aingie madarakani nchini Marekani; na hakuna mkutano wowote uliofanywa hadi sasa kati ya marais wa nchi mbili za Russia na Marekani.
Kwa mujibu wa ripoti hii, miezi 6 na siku 16 zimepita tangu Rais Donald Trump ahudumu katika muhula wake wa pili, na hakuna mkutano wowote aliofanya na Rais Vladimir Putin wa Russia.
Wakati wa kampeni zake za urais, Trump alionyesha nia ya kuboresha uhusiano na Russia. Trump ametaja mkutano kati yake na Putin kuwa muhimu, lakini ikulu ya Russia (Kremlin) imesema kuwa pande mbili zinapasa kufanya kazi kubwa ili kukutana marais wa nchi mbili.