Maandamano nchini Uingereza yataka kukamatwa Rais wa Israel
Maandamano makubwa yamefanyika nchini Uingereza ambapo waandamanaji wametoa wito wa kukamatwa Rais wa Israel kwa kutenda jinai huko Palestina.
Waandamanaji walipaza sauti zao nje ya Chatham House mjini London, ambapo Rais wa Israel Isaac Herzog alihutubia wajumbe kutoka Kituo cha Utafiti wa Masuala ya Kimataifa.
Waandamanaji waliimba nara za kuunga mkono Gaza, wakipeperusha bendera za Palestina na kutaka Rais wa Israel Isaac Herzog atiwe mbaroni na kuushtakiwa kwa Kutenda jinai dhidi ya Wapalestina.
Isaac Herzog alikutana na Waziri Mkuu wa Uingereza Keir Starmer katika Mtaa wa Downing wakati wa ziara rasmi ya siku tatu nchini Uingereza.
Ziara hiyo imekuja baada ya Downing Street kulaani mashambulizi ya anga ya Israel katika mji mkuu wa Qatar, Doha, yakiwalenga viongozi wa Harakati ya Mapambano ya Kiislamu ya Palestina HAMAS.
Mazungumzo hayo yanajiri huku kukiwa na maandamano yanayoendelea dhidi ya utawala wa kizayuni wa Israel, huku mzozo wa kibinadamu huko Gaza ukiongezeka kutokana na vita vinavyoendelea kufanywa na Israel katika Ukanda huo.
Mashinikizo na chuki dhidi ya viongozi wa Israel zinazidi kuongezeka katika kila kona ya dunia ikiwa ni matokeo ya jinai za utawala huko dhidi ya Wapalestina.
Rais wa Croatia Zoran Milanovic siku ya Jumanne alikataa kukutana na Waziri wa Mambo ya Nje wa Israel Gideon Saar wakati wa ziara yake rasmi huko Zagreb akitaja mauaji ya Israel huko Gaza kama sababu ya kukataa kukutana na mwanadiplomasia huyo wa Israel.