Umoja wa Mataifa: Hatua ya Trump inakiuka sheria za kimataifa
Kamisheni Kuu ya Haki za Binadamu ya Umoja wa Mataifa imetangaza kuwa, amri iliyotiwa saini na Rais Donald Trump wa Marekani ya kuzuia raia wa nchi saba za Kiislamu kuingia nchini Marekani ni kinyume cha sheria za kimataifa.
Kamishna wa Haki za Binadamu wa Umoja wa Mataifa, Zeid Ra’ad Zeid al-Hussein amesema kuwa ni marufuku na kinyume cha sheria kuwabagua watu kwa mujibu wa utaifa wao.
Ra’ad al-Hussein ameongeza kuwa, sheria ya kuwazuia Waislamu kuingia nchini Marekani iliyoanza kutekelezwa Marekani ni ya kikatili na sababu ya kuharibiwa rasilimali zinazohitajika kwa ajili ya kupambana ipasavyo na ugaidi.
Msimamo huo wa Kamishna wa Haki za Binadamu wa Umoja wa Mataifa umetangazwa baada ya Rais Donald Trump wa Marekani kusaini amri inayowazuia raia wa nchi kadhaa za Kiislamu kuingia nchini humo.
Hatua hiyo ya Trump anayejulikana kwa fikra na misimamo yake ya kibaguzi hususan dhidi ya Waislamu na wahamiaji, imekosolewa sana na nchi na jumuiya mbalimbali za kimataifa za kutetea haki za binadamu.