Guterres: Wote watimize ahadi ya kutokomeza dawa za kulevya
Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa ametoa wito kwa ushirikiano wa kimataifa katika kupunguza biashara, matumizi na madhara ya matumizi ya madawa ya kulevya.
António Guterres ameyasema hayo katika ujumbe wake kwa munasaba wa siku ya kimataifa ya kupinga matumizi ya madawa ya kulevya ambayo inaadhimishwa Jumatatu Juni 26.
Guterres amesema, kutokana na uzoefu wake anafahamu jinsi tahadhari na tiba vinaweza kuleta matokeo mujarabu akitolea mfano nchi yake Ureno wakati alipokuwa waziri mkuu ambako kwa sasa ni nchi yenye idadi ndogo zaidi ya vifo vinavyotokana na matumizi ya mihadarati barani Ulaya.
Licha ya changamoto zinazokabili utatuzi wa tatizo hilo la kimataifa, Katibu Mkuu huyo amesema anatumai na kuamini kwamba dunia iko katika njia sahihi na kwa pamoja kuna uwezekano wa kutekeleza mbinu muafaka ambazo zitazaa matokeo endelevu.