Rais wa Ukraine: Kuna uwezekano tukaingia vitani na Russia
Sambamba na Rais Petro Poroshenko wa Ukraine kusema kuwa, Russia imeimarisha zaidi kuwepo kwake kijeshi katika mpaka wa nchi hiyo, ameeleza kuwa, kuna uwezekano kukatokea vita kamili kati ya nchi yake na Russia.
Kwa mujibu wa Poroshenko, idadi ya vifaru vya Russia katika vituo vya kijeshi vya nchi hiyo vilivyoko kwenye mpaka wa pamoja wa nchi mbili imeongezeka mara tatu zaidi. Aidha Rais wa Ukraine ameongeza kwamba mbali na vifaru, Russia imezidisha idadi ya meli za kivita katika maji ya bahari ya Azov na katika kisiwa cha Crimea ambacho miaka minne iliyopita kiliunganishwa na Russia. Sambamba na kulichukulia suala hilo kwa umuhimu mkubwa, amesema kuwa ni tishio la kivita linalotolewa na Moscow kwa nchi yake.
Amezidi kufafanua kwamba, Jumanne asubuhi alitaka kuongea na Rais Vladimir Putin wa Russia lakini rais huyo hakumjibu na badala yake akalazimika kumuomba, Kansela Angela Merkel wa Ujerumani azungumze na kiongozi huyo wa Russia. Jumapili iliyopita meli tatu za Ukraine zilivuka lango la Kerch lililopo kati ya Bahari Nyeusi na Bahari ya Azov na kuingia katika maji ya Russia ya kisiwa cha Crimea hatua ambayo ilipelekea kuibuka mapigano ya meli za kivita kati ya nchi mbili. Aidha jeshi la Russia lilizisimamisha meli hizo za Ukraine na kuzikagua.