Feb 08, 2023 01:02 UTC
  • Jumatano, tarehe 8 Februari, 2023

Leo ni Jumatano, tarehe 17 Rajab 1444 Hijria sawa na Februari 8 mwaka 2023.

Miaka 323 iliyopita katika siku kama ya leo ya tarehe tarehe 17 Rajab, alifariki duani Allamah Fadhil Sheikh Sulaiman Bahrani, aliyekuwa miongoni mwa wasomi wakubwa wa Kishia.

Sheikh Abul-Hassan Sulaiman Ibn Abdillah Ibn Ali Ibn Hassan Bahrani Mahuzi, maarufu kwa jina la Muhaqqiq Bahrani, mmoja wa maulama wa Kishia wa mwanzoni mwa karne ya 12 Hijiria, alizaliwa katikati ya mwezi wa Ramadhani mwaka 1076 Hijiria. Alibobea katika elimu ya hadithi, wapokezi wa Hadithi, historia na maisha ya mtukufu Mtume (saw) na Ahlu Baiti wake (as). Sheikh Abdullah Samahiji na Sayyid Hashim Bahrani, mwandishi wa tafsiri ya Qur'ani ya Al-Burhan na Sheikh Ahmad Bahrani, ni miongoni mwa wanafunzi wa Allamah Fadhil Sheikh Sulaiman Bahrani.

Miongoni mwa athari zake ni pamoja na kitabu cha 'al-Shifaau fil-Hikmat al-Nadharia wal-Mi'raaj.' Msomi huyo mkubwa alifariki dunia akiwa na umri wa miaka 46. ***

Katika siku kama ya leo miaka 173 iliyopita, kulingana na kalenda ya Hijria, Sayyid Abu-Turab Khansari, mmoja wa maulama na maustadhi wakubwa alizaliwa huko Khansar moja kati ya miji ya katikati mwa Iran.

Ayatullahil Udhma Khansari alisoma masomo ya teolojia na Hadithi kwa walimu mashuhuri wa zama zake. Juhudi zake masomoni zilimfanye aondokee kuwa ustadhi mahiri katika masomo ya fiqhi, usulul fiqhi na tafsiri ya Qur'ani.

Ayatullah Khonsari ameandika vitabu vingi kuhusiana na elimu mbalimbali za kidini. Kitabu cha Qasdus Sabil kuhusiana na elimu ya usulul fqhi na Misbahus Swalihiin kinachozungumzia misingi ya dini, ni baadhi tu ya vitabu vyenye thamani vya msomi huyu mahiri wa Kiislamu aliyefariki dunia mwaka 1346 Hijria.

Sayyid Abu-Turab Khansari

Katika siku kama hii ya leo miaka 50 iliyopita Abdu Salam Arif alifanikiwa kushika hatamu za uongozi nchini Iraq, baada ya kufanya mapinduzi ya umwagaji damu akishirikiana na maafisa wa jeshi wa Chama cha Baath.

Akisaidiwa na majeshi ya anga ya Iraq, Kanali Abdu Salam Arif alilishambulia jengo la Wizara ya Ulinzi ya Iraq yalipokuwa makao ya Abdul-Karim Qassim, Rais wa wakati huo wa nchi hiyo. Baada ya kumtia mbaroni na kumuua Rais huyo, Abdu Salam Arif alijitangaza kuwa Rais wa nchi hiyo.

Abdul-Karim Qassim alikuwa ameingia madarakani mwaka 1958, baada ya kufanya mapinduzi ya umwagaji damu dhidi ya mfalme wa mwisho wa Iraq.

Kanali Abdul Salam Arif alifariki dunia mwaka 1966 katika tukio la kutatanisha la ajali ya helikopta, na kaka yake yaani Abdul-Rahman Arif akawa Rais wa Iraq.

Abdu Salam Arif

Siku kama ya leo miaka 43 iliyopita wananchi wa Iran walifanya maandamano makubwa katika miji mbalimbali ya Iran na kusisitiza juu ya kuendelezwa mapambano hadi kuuangusha utawala wa Shah.

Mamilioni ya wananchi Waislamu wa Iran waliandamana katika siku kama hii wakijibu wito wa Imam Khomeini Mwenyezi Mungu amrehemu aliyewataka waiunge mkono serikali ya muda ya Mapinduzi.

Katika upande mwingine maafisa na vikosi vya Jeshi la Anga la Iran waliokuwa katika sare zao za kijeshi, walielekea kwa Imam na kutangaza mshikamano wao na Mapinduzi ya Kiislamu na uongozi wa Imam Ruhullah Khomeini. Katika mazungumzo hayo, Imam Ruhullah Khomeini aliwaambia wanajeshi hao kwamba walikuwa watumishi wa utawala wa kitaghuti na sasa wamejiunga na Qur'ani.

Hatua ya vikosi vya Jeshi la Anga la Iran ya kutangaza utiifu wao kwa Imam Khomeini iliukasirisha sana utawala wa Shah.

Maafisa wa Jeshi la Anga la Iran