Oct 05, 2023 14:01 UTC
  • Somalia: Tumeua wanachama 1,650 wa al-Shabaab ndani ya miezi 2

Serikali ya Somalia imesema imefanikiwa kuangamiza wanachama 1,650 wa kundi la kigaidi la al-Shabaab katika operesheni za vikosi vya jeshi la nchi hiyo katika kipindi cha miezi miwili iliyopita.

Shirika rasmi la habari la Somalia (SONNA) limetangaza habari hiyo na kuongeza kuwa, makamanda 19 wa ngazi za juu wa al-Shabaab ni miongoni mwa mamia ya wanachama wa genge hilo walioangamizwa katika operesheni hizo.

Kwa mujibu wa shirika la habari la Anadolu, hii ndiyo idadi kubwa zaidi ya kuuawa al-Shabaab kuwahi kutangazwa na serikali ya Somalia, tangu awamu mpya ya operesheni za kulitokomeza kundi hilo ilipoanza mwishoni mwa mwaka uliopita.

Haya yanajiri siku moja baada ya Kikosi cha Mpito cha Umoja wa Afrika nchini Somalia (ATMIS) kusema kuwa askari wake kutoka Burundi na Uganda wamefanya operesheni ya pamoja wakishirikiana na wanajeshi wa Somalia na kutoa pigo kubwa dhidi ya wanachama wa kundi la al-Shabaab.

Maiti za wanamgambo wa al-Shabaab

Duru za habari zinaarifu kuwa, operesheni hiyo ya pamoja ya askari wa AU imefanyika katika eneo la Ali Foldhere, katika mkoa wa kusini magharibi wa Middle Shabelle.

Haya yanajiri siku chache baada ya Jeshi la Ulinzi la Taifa la Ethiopia (ENDF) kusema kuwa limeua wanachama 462 wa kundi la kigaidi la al-Shabaab katika mji wa Rabdhure, kusini magharibi mwa Somalia. 

Operesheni hizo dhidi ya al-Shabaab zimeshtadi wakati huu ambapo Umoja wa Afrika unaendelea na awamu ya pili ya kuondoa wanajeshi wa umoja huo (ATMIS) kutoka nchi hiyo ya Pembe ya Afrika. 

Tags