Al-Azhar yawataka Waarabu na Waislamu kupinga kufukuzwa Wapalestina Gaza
Chuo Kikuu cha Kiislamu cha al-Azhar nchini Misri kimesisitiza kwa mara nyingine tena juu ya kupinga mpango wa kufukuzwa Wapalestina wa Gaza kutoka katika ardhi yao na kuwataka Waarabu na Waislamu kujitokeza na kupinga mpango huo.
Chuo Kikuu cha Kiislamu cha al-Azhar nchini Misri kimetoa mwito kuungwa mkono misimamo ya Misri na mataifa mengine ya Kiarabu katika ujenzi na ukarabati mpya wa Ukanda wa Gaza bila ya kuondolewa wakazi wake.
Sehhemu nyingine ya taarifa ya al-Azhar imebainisha kwamba, inaunga mkono suala la kuijenga na kuikarabati Gaza, lakini kwa sharti kwamba Wapalestina wasalie katika eneo hilo na kuongezwa mashinikizo ya kutekelezwa makubaliano ya usitishaji vita katika Ukanda wa Gaza.
Kadhalika imewataka viongozi wote wa Kiarabu na Kiislamu kupinga mpango wa kuwafukuza Wapalestina, ambao imesema lengo lake kufuta kabisa kadhia ya Palestina kwa kuwalazimisha Wapalestina kuondoka katika ardhi yao, ambayo wameishi kwa maelfu ya miaka.
Rais wa Marekani, Donald Trump, amekariri bila ya aibu pendekezo lake tata la kulinyakua na kulidhibiti eneo la Ukanda wa Ghaza, akisema amejitolea "kulinunua na kulimiliki" eneo hilo lililoharibiwa na vita uamuzi ambao umeibua upinzani mkali katika kila kona yay a ulimwengu wa Kiislamu na Kiarabu.