Niger yajitoa rasmi katika Jumuiya ya Nchi Zinazozungumza Kifaransa, Francophone
(last modified Wed, 19 Mar 2025 04:14:22 GMT )
Mar 19, 2025 04:14 UTC
  • Niger yajitoa rasmi katika Jumuiya ya Nchi Zinazozungumza Kifaransa, Francophone

Niger imejiondoa rasmi katika Jumuiya ya Kimataifa ya nchi zinazozungumza Kifaransa (OIF) au Francophone sambamba na juhudi zinazoendelea kufanywa na taifa hilo la Afrika Magharibi za kuvunja uhusiano na kujitenga na mkoloni wake wa zamani, Ufaransa.

Hayo yameelezwa katika taarifa iliyotolewa na Wizara ya Mambo ya Nje ya Niger.
"Serikali ya Waniger imeamua kwa uhuru kuiondoa Niger katika Shirika la Kimataifa la Francophonie," imeeleza wizara hiyo katika ujumbe uliotumwa kwenye mtandao wa kijamii wa X.
Hatua hiyo imechukuliwa baada ya kupita zaidi ya mwaka mmoja tangu utawala wa kijeshi wa Niamey kusimamisha kila aina ya ushirikiano na shirika la Francophone lenye makao yake makuu mjini Paris, likilituhumu kuwa chombo cha kisiasa cha kutetea maslahi ya Ufaransa.

Baraza la Kudumu la wanachama 88 wa OIF lilisimamisha uanachama wa Niger mwezi Desemba 2023 miezi kadhaa baada ya mapinduzi ya kijeshi ya Julai mwaka huo ambayo yalimuondoa madarakani rais wa zamani Mohamed Bazoum. Uamuzi huo wa OIF ulichukuliwa ili kuushinikiza uongozi mpya wa kijeshi kurejesha utawala wa katiba nchini Niger.

Baraza hilo la Jumuiya ya Kimataifa ya nchi zinazozungumza Kifaransa lilitangaza kuwa litaendeleza ushirikiano na Niger katika miradi ambayo inanufaisha raia moja kwa moja na kuchangia katika kurejesha demokrasia katika koloni hilo la zamani la Ufaransa.

Hata hivyo tangu iliposhika hatamu za uongozi wa nchi, serikali ya kijeshi ya Niger, inayojulikana kama Baraza la Kitaifa la Kulinda Nchi, imechukua hatua kadhaa za kukata uhusiano na Paris, ikiwa ni pamoja na kuwafukuza wanajeshi wa Ufaransa waliokuwa na vituo vya kijeshi nchini humo.../