Nigeria yawafunga watu 44 waliofadhili kundi la kigaidi la Boko Haram
https://parstoday.ir/sw/news/africa-i128280-nigeria_yawafunga_watu_44_waliofadhili_kundi_la_kigaidi_la_boko_haram
Serikali ya Nigeria imewahukumu watu 44 kifungo cha hadi miaka 30 jela kwa makosa ya kufadhili ugaidi, msemaji wa shirika la kupambana na ugaidi nchini humo amebaini.
(last modified 2025-07-13T10:28:06+00:00 )
Jul 13, 2025 10:28 UTC
  • Nigeria yawafunga watu 44 waliofadhili kundi la kigaidi la Boko Haram

Serikali ya Nigeria imewahukumu watu 44 kifungo cha hadi miaka 30 jela kwa makosa ya kufadhili ugaidi, msemaji wa shirika la kupambana na ugaidi nchini humo amebaini.

Waliohukumiwa walikuwa miongoni mwa washukiwa 54 walioshtakiwa mbele ya mahakama nne maalum zilizoundwa kwa ajili ya raia, zikiwa ndani ya kambi ya kijeshi mjini Kainji, katika jimbo la Niger katikati mwa Nigeria.

Kwa mujibu wa Abu Michael, msemaji wa Kituo cha Kitaifa cha Kupambana na Ugaidi cha Nigeria, kesi za washukiwa wengine 10 ziliahirishwa hadi tarehe nyingine.

Nigeria ilianza tena kusikiliza kesi hizo Jumatano, baada ya kusitisha kwa zaidi ya miaka saba mashitaka dhidi ya zaidi ya watu 1,000 waliokuwa wakishukiwa kuwa na uhusiano na kundi la kigaidi la Boko Haram, ambalo limekuwa likihusika na mashambulizi ya kikatili tangu mwaka 2009.

Michael amesema maamuzi yaliyotolewa katika kesi hizo yalisababisha hukumu za kifungo cha miaka 10 hadi 30 na kazi ngumu.

Taarifa hiyo imeongeza kuwa: “Kwa hukumu hizi mpya, Nigeria sasa imeshughulikia jumla ya kesi 785 zinazohusiana na ufadhili wa ugaidi na uhalifu mwingine wa kigaidi.”

Ghasia za Boko Haram, zilizoanzia kaskazini-mashariki mwa Nigeria, zimevuka mipaka na kuathiri mataifa jirani ya Cameroon, Chad na Niger—zikisababisha vifo vya maelfu ya watu na kuwalazimisha mamilioni kukimbia makazi yao.

Kwa miaka kadhaa, maelfu ya wapiganaji wa Boko Haram pamoja na familia zao wamejisalimisha kwa jeshi la Nigeria, huku operesheni za kijeshi dhidi yao zikiimarishwa.