Serikali ya Msumbiji yaomba msaada wa haraka wa kimataifa kufuatia mafuriko makubwa
https://parstoday.ir/sw/news/africa-i135832-serikali_ya_msumbiji_yaomba_msaada_wa_haraka_wa_kimataifa_kufuatia_mafuriko_makubwa
Serikali ya Msumbiji imeomba Ijumaa kwamba jumuiya ya kimataifa ichukue hatua za dharura za kibinadamu ili kukabiliana na mafuriko makubwa ambayo yamesababisha maelfu kwa maelfu kuyahama makazi yao na kuharibu miundombinu katika taifa hilo la Kusini Mashariki mwa Afrika.
(last modified 2026-03-27T07:58:19+00:00 )
Jan 24, 2026 04:24 UTC
  • Mafuriko msumbiji
    Mafuriko msumbiji

Serikali ya Msumbiji imeomba Ijumaa kwamba jumuiya ya kimataifa ichukue hatua za dharura za kibinadamu ili kukabiliana na mafuriko makubwa ambayo yamesababisha maelfu kwa maelfu kuyahama makazi yao na kuharibu miundombinu katika taifa hilo la Kusini Mashariki mwa Afrika.

Taasisi ya Kitaifa ya Usimamizi wa Majanga (INGD) ilisema kuwa Msumbiji inakabiliwa na mafuriko mabaya zaidi kuwahi kutokea kwa miongo kadhaa, ambayo, kwa mujibu wa takwimu, yamewalazimu watu 600,000 kuyahama makazi yao katika mikoa iliyoathirika zaidi ya Gaza, Zambezia, Inhambane na Sofala. Takribani asilimia 40 ya Mkoa wa Gaza inasemekana kuwa chini ya maji. Wiki kadhaa za mvua kubwa mfululizo zimechochea mafuriko ya kutisha Kusini mwa Afrika na kusababisha vifo vya watu wengi.

Gabriel Monteiro, makamu mwenyekiti wa INGD, amewaambia waandishi wa habari kwamba rasilimali za nchi “hazitoshi kukabiliana na janga la ukubwa huu.”

Monteiro amesema, “Hadi sasa, tuna washirika kutoka maeneo mbalimbali duniani ambao wamekuja kutusaidia, lakini ukubwa wa tukio hili unazidi mipango yetu yote. Hivyo basi, tunaomba msaada wa kibinadamu kutoka kote duniani ili kudhibiti athari mbaya za mafuriko haya.”

Serikali imesema kuwa takribani watu 13 wamethibitishwa kufariki, huku wengine wengi wakiripotiwa kutoweka katika kipindi cha wiki mbili zilizopita.

Mary Louise Eagleton, mwakilishi mkazi wa UNICEF nchini humo, amewaambia waandishi wa habari kuwa idadi ya vifo inaweza kuongezeka.

Amesema, “Tunatarajia pia kuona kwamba sehemu kubwa ya wale waliosombwa na maji ni watoto. Kwa hiyo, tunafanya kazi kubaini idadi kamili ya waliopoteza maisha.”

Serikali ya Afrika Kusini imetuma wanajeshi Msumbiji ili kuimarisha shughuli za uokoaji. Monteiro alisema kuwa jamii zilizopoteza makao zinakabiliwa na upungufu mkubwa wa makazi pamoja na mahitaji muhimu kama maji, huduma za usafi na chakula. Msumbiji ilikumbwa na mafuriko makubwa mwaka 2000, yaliyosababisha vifo vya takribani watu 1,000.